Saturday, June 8, 2013

Wasomali wakataa madai ya al-Shabaab juu ya chanjo ya polio

Kwa zaidi ya wiki mbili, wanamgambo wa al-Shabaab walishindwa kuzuia kampeni ya kitaifa inayoongozwa na serikali ya kuwakinga watoto dhidi ya polio, maafisa wa afya ya umma walisema.
Kama sehemu ya kampeni ya propaganda hiyo, wanamgambo walivamia mitaa katika maeneo wanayoyadhibiti ya Bulo Barde, Buale na Baardheere, wakieneza uongo kuhusu chanjo hiyo ili kuwatisha wazazi.
"Chanjo hii ni ajenda ya nchi za Magharibi dhidi ya Waislamu," wanamgambo walisema kwa kutumia vipaza sauti katika magari yaliyokuwa yanazungukazunguka, kwa mujibu wa Abdinur Dahir, mkaazi wa Bulo Barde mwenye umri wa miaka 46.
"Chanjo hii ina vitu vyenye sumu ambavyo vinaweza kuwafanya watoto wasiwe na uwezo wa kuzaa," wanamgambo hao walisema. "Chanjo hii ina virusi vinavyosababisha UKIMWI. Wakingeni watoto wenu!"
Vikundi vyengne vyenye uhusiano na al-Qaida vimeeneza proaganda kama hiyo inayolenga kampeni ya chanjo huko Afghanistan na Pakistan ya kuwakinga watoto dhidi ya polio, ugonjwa uliotokomezwa kwa kiasi kikubwa lakini unaoambukiza sana na inayoweza kusababaisha kupooza kusikotibika.
Wasomali wengi hata hivyo, walikataa kuamini madai ya al-Shabaab kuhusu hatari za chanjo hiyo.
Kwa kweli, familia nyingi ziliipokea vizuri kampeni hiyo na kukusanyika kwa makundi makubwa ili watoto wao wachanjwe, Yasin Nur alisema, afisa wa mpango wa chanjo katika Idara ya Afya kwenye Wizara ya Maendeleo na Masuala ya Jamii.
"Mahitaji haya makubwa kwa upande wa wazazi kuwachanja watoto wao kunadhihirisha kwamba madai ya kupotosha yaliyofanywa na al-Shabaab yameangukia patupu," Nur aliiambia Sabahi.
Serikali ya Somalia ilianzisha kampeni ya awamu mbili ya kuzuia polio katikati ya mwezi wa Mei baada ya kesi nne za polio kuthibitishwa katika miezi sita iliyopita. Awamu ya kwanza ya kampeni hiyo, kuanzia tarehe 14 hadi 18 mei, ilikusudiwa kuwachanja zaidi ya watoto 440,000 wenye umri wa miaka 10 na chini ya hapo. Awamu ya pili, kuanzia tarehe 28 Mei hadi tarehe 2 Juni, iliwalenga zaidi ya watoto 640,000 wa kundi la umri huo huo, Nur alisema.
Wizara ya Maendeleo na Masuala ya jamii iliendesha kampeni hiyo kwa msaada wa Shirika la Afya Duniani na Mfuko wa Watoto wa Umoja wa Mataifa (UNICEF), Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Uratibu wa Masuala ya Kibinadamu na mashirika mengine yasiyo ya kifaida.

Kushirikiana na vingozi wa jamii, kuwaelimisha wazazi

Katika kuelekea kwa kampeni hiyo ya chanjo, viongozi wa maeneo na viongozi wa kikabila na kidini waliendesha kampeni za matangazo ili kuzishawishi jamii kupuuza uvumi wa al-Shabaab na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa kuwachanja watoto wao dhidi ya polio.
Isaaq Aadan, ambaye aliratibu kampeni katika mikoa ya Bay na Bakool, alitathmini kampeni ya matangazo huko kuwa ya mafanikio.
"Juhudi za mwamko za kuzihamasisha jamii kuhusu umuhimu wa chanjo hii zilisababisha familia nyingi kukubali kuchanja watoto wao kwa kuwa viongozi wa jamii, viongozi wa kidini na kambi za watu wa ndani waliokimbia makazi yao (IDP) waliwataka watu kutumia fursa ya chanjo hiii," Aadan alisema.
Kabla ya kampeni hiyo ya chanjo, timu za kuhamasisha jamii pia zilifanya matembezi ya nyumba kwa nyumba ili kuwataka wazazi wasiamini madai ya uongo yanayofanywa na al-Shaabab, alisema. Wafanyakazi wa afya waliwaamba wazazi kuhusu madhara ya kuambukizwa na polio na kwamba njia pekee ya kuwakinga watoto wao ni kupitia chanjo.
"Licha ya propaganda na uvumi ambao umekuwa ukienezwa na al-Shabaab dhidi ya chanjo ya polio, mpaka hivi sasa tumeshuhudia maendeleo kwa kiasi kikubwa kwa vile familia nyingi zimefahamu umuhimu wa kuwachanja watoto wao na ndio maana walizipokea timu za chanjo wakati wa kampeni," Aadan alisema.

Polio inasambaa katika maeneo yanayodhibitiwa na al-Shabaab

Kampeni za chanjo zilifikia maeneo makubwa nchini na kuwafikia mamia ya watoto ambao huko nyuma walikuwa hawapati chanjo ya polio. Al-Shabaab hata hivyo, walipiga marufuku kampeni za chanjo katika maeneo yao wanayoyadhibiti na kuwazuia wafanyakazi wa chanjo wasiwafikie.
Marufuku hiyo inayaweka maisha ya watoto hatarini, wafanyakazi wa afya walisema.
"Ingawa kufukuzwa kwa kikundi hicho chenye msimamo mkali cha al-Shabaab kutoka miji mikuu ya kati na kusini ya Somalia kumewasaidia wafanyakazi wa afya kuwafikia watoto zaidi na zaidi na kuwapa chanjo ya polio ... virusi vya polio vinasambaa katika maeneo chini ya udhdibiti wa al-Shabaab kwa hivyo kuwa vigumu kuweza kuwafikia watoto [katika maeneo hayo]," alisema Said Yussuf, mfanyakazi wa chanjo.
Amina Mohamed, mama mwenye umri wa miaka 34 ambaye anaishi katika Kambi ya Tawakal mjini Mogadishu, aliwapeleka watoto wake wote kwa ajili ya kuchanjwa.
"Nimesikia kwamba al-Shabaab wanawataka akina baba na akina mama wote wasiwachanje watoto wao kwa misingi kwamba chanjo hii imetengenezwa na nchi za Kikristo, na ina vitu vya sumu ambavyo vingeweza kuwasababishia watoto kutoweza kuzaa watakapokuwa wakubwa," Mohamed alisema.
"[Wafanyakazi wa chanjo] walituambia kwamba madai haya na uvumi zilizopangwa na al-Shabaab ni sehemu ya propaganda [za kuchanganyikiwa] kwa kikundi hicho kwa ajili ya lengo lao la bure kwa gharama ya afya ya watoto wetu," alisema. "Kwa kweli, tunaelewa kwamba al-Shabaab hawako sahihi na kwamba ni kikundi kinachotumia picha potofu ya dini na kwamba madai na uvumi wanazosambaza zimeundwa ili kuwapotosha watu wa Somalia. Kwa sababu hii, tunakataa kukubali madai hayo dhaifu yanayoundwa na al-Shabaab."

Rasimu ya Katiba chungu kwa CCM

Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete akiwa na viongozi wenzake wakati wa kikao chake na wabunge wa CCM, mnamo Mei 19, 2013, katika ukumbi wa jengo la White House, Dodoma. CCM imetangaza kufanya mkutano wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa  ili kuichambua na kujadili kwa kina rasimu ya Katiba Mpya.
Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete akiwa na viongozi wenzake wakati wa kikao chake na wabunge wa CCM, mnamo Mei 19, 2013, katika ukumbi wa jengo la White House, Dodoma. CCM imetangaza kufanya mkutano wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ili kuichambua na kujadili kwa kina rasimu ya Katiba Mpya.
Mwanzoni mwa wiki hii Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilizindua rasimu ya Katiba Mpya iliyopendekeza kuwapo kwa mabadiliko makubwa kwenye mfumo wa utawala nchini, huku yakionekana kuwa machungu kwa chama tawala cha CCM.
Tayari CCM kimetangaza kufanya mkutano wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho ili kuichambua na kujadili kwa kina rasimu hiyo ya Katiba Mpya.
Jana vyombo vya habari vilimnukuu Katibu Mkuu wa chama hicho Abdulrahman Kinana katika mkutano wake na waandishi wa habari akisema kuwa wataichambua na kuijadili rasimu hiyo.
Pamoja na mambo mengine, rasimu hiyo ya Katiba Mpya imependekeza kuwapo kwa Serikali tatu; Shirikisho la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Tanzania Bara na Serikali ya Zanzibar, kuruhusiwa kwa mgombea binafsi na kufutwa kwa viti maalumu vya ubunge.
Mapendekeo hayo yametolewa ikiwa ni miezi sita tangu vyama mbalimbali vya siasa kuwasilisha maoni yao kwa tume hiyo inayoongozwa na Jaji Joseph Warioba na kupendekeza mambo mbalimbali ikiwamo muundo wa Serikali, Uchaguzi Mkuu na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).
Mapendekezo ya CCM
Katika mapendekezo yake CCM walitaka ubaki mfumo wa Serikali mbili kama ilivyo sasa, ikieleza kuwa hauna gharama, huku kikieleza kwamba uzoefu katika nchi nyingi za Afrika unathibitisha kushindwa kwa mfumo wa Serikali tatu na ule wa Serikali ya Shirikisho (Federation government).
Hata hivyo, mapendekezo ya rasimu hiyo yanaonyesha kuwa Jamhuri ya Muungano itakuwa na muundo wa shirikisho lenye Serikali tatu na kwamba shughuli zote za muungano zitasimamiwa na Serikali, Bunge na Mahakama ya Jamhuri ya Muungano, hivyo kukifanya CCM kuanguka katika maoni kuhusu suala hilo.
CCM ilipendekeza sera ya dola kutokuwa na dini rasmi, bali iruhusu kila mtu kuwa na uhuru wa kufuata dini anayoitaka mwenyewe, jambo ambalo limebaki kama lilivyo katika mapendekezo ya rasimu hiyo.
Chama hicho kimeonekana kukwama pia katika mapendekezo yake ya kuupigia debe mfumo wa sasa wa rais kushinda kwa wingi wa kura (simple majority) kwa maelezo kuwa hauna gharama pamoja na kutaka wananchi wawe na haki ya kuhoji uchaguzi wa rais.
Lakini, mapendekezo katika rasimu hiyo yanaeleza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano atatangazwa baada ya kupata zaidi ya asilimia 50 ya kura zote na endapo hakutakuwa na mshindi, walioshika nafasi ya kwanza na ya pili watarudia uchaguzi ndani ya siku 60.
CCM kilipendekeza mawaziri wasitoke nje ya Bunge, huku kikitaka kuongezwa kwa wigo wa viongozi wanaoteuliwa na rais na kupitishwa na Bunge kama ilivyo kwa waziri mkuu.
Mapendekezo mengine ya chama hicho ambayo hayakupitishwa ni kuanzishwa kwa utaratibu utakaoshirikisha Bunge katika uteuzi wa baadhi ya vyombo vya utendaji ikiwemo tume ya uchaguzi na kutokuwepo mgombea binafsi .
Mbali na hayo, chama hicho pia kilitaka uwepo ukomo wa idadi ya wabunge ili kuzuia uwezekano wa kuongeza majimbo bila kuzingatia vigezo mahsusi na uwezo wa taifa.
Kuhusu wabunge wa viti maalumu CCM ilitaka idadi ya wabunge hao itokane na asilimia ya idadi ya viti iliyopata chama baada ya kushinda uchaguzi.
Kuhusu kuhoji mahakamani matokeo ya uchaguzi wa rais, CCM ilitaka uwepo utaratibu maalumu wa kupinga matokeo hayo na siyo mahakamani.
Chadema
Kwa upande wa Chadema kilipendekeza kuanzishwa kwa utawala wa majimbo yasiyozidi kumi ili kuleta uwiano katika matumizi ya rasilimali kwenye maeneo yote ya nchi. Hata hivyo, rasimu hiyo ilipendekeza kutokuwepo kwa Serikali za majimbo ikieleza kungechochea mgawanyiko ambao ungejengwa kwa misingi ya udini, ukabila na ukanda.
Chadema pia kilipendekeza umri wa kugombea ubunge ushushwe hadi miaka 18 ili kutoa nafasi kwa mtu yoyote kuwa na haki ya kupiga au kupigiwa kura, lakini rasimu hiyo imeeleza kuwa umri wa mtu kugombea ubunge ni miaka 21 huku ikitaja umri wa kugombea urais kuwa ni kuanzia miaka 40.
Kwa upande wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) chama hicho kilipendekeza iwe na wajumbe 25 kati yao 15 watokane na vyama vyenye uwakilishi bungeni na wateuliwa kwa uwiano wa wabunge walioko bungeni, wengine watoke kwenye asasi za kiraia, vyama vya wakulima, jumuiya za kidini na vyama vingine vya siasa visivyo na uwakilishi bungeni na mwenyekiti na makamu wake wateuliwe na wajumbe wenyewe.
Katika hilo chama hicho kimekwama kwani rasimu imependekeza kuwa wajumbe wa tume hiyo watateuliwa na rais.
Mapendekezo ya chama hicho ambayo yamepitishwa na tume ni pamoja na kuwepo kwa Serikali tatu, matokeo ya urais kuhojiwa mahakamani.
CUF
Ilipendekeza kuwapo Katiba tatu zitakazoongoza Serikali za Tanganyika, Zanzibar na Muungano jambo ambalo limependekezwa pia na Rasimu ya Katiba Mpya.
Chama hicho pia kilipendekeza mgombea binafsi katika nafasi ya urais, kupunguzwa kwa madaraka ya rais na rais apatikane kwa kupata zaidi ya asilimia 50.

Kuongoza watu kwa ulimi badala ya maarifa

Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai
Na Jabir Idrissa
VIONGOZI waandamizi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa Zanzibar kwa kweli wanachekesha kwa namna wanavyotunisha misuli ya shingo kupinga utashi wa wananchi wa Zanzibar kutaka mabadiliko ya mfumo wa muungano wao na Tanganyika. Waelewe kuwa suala la Wazanzibari kudai kurudishwa mamlaka iliyokuwa nayo serikali baada ya uhuru wa 10 Desemba, 1963 ni haki yao isiyopingika. Hata kama mtu atapinga, bado haki ya kutaka watakacho wananchi haitafutika.
Muungano wowote, hata wa watoto unapaswa kuwa endelevu. Unapaswa kuendeshwa kwa kuzingatia haki kwa walioungana. Watoto walioungana watapendana. Lakini upendo kwao utakuwa na maana tu iwapo watachangia kwa usawa kile walichokubaliana.
Utasikia Khadija lete mchele. Haya naleta lakini wewe lete nazi. Naye atasema sawa, lakini na Riziki yeye alete kuni za kupikia. Riziki ataridhia kuleta kuni. Ila naye atasema Mariam alete chumvi. Watatajana hivyo katika utaratibu wa kuchangia mpaka wahakikishe chakula kitapikika. Kikiwiva watakula pamoja. Hao ni watoto, itakuwa watu wazima walioungana?
Kilio cha Wazanzibari tangu Muungano ulipoasisiwa mwaka 1964 ni kutokuwepo kwa nia njema. Hazikupita siku nyingi, muasisi mmojawapo, Mzee Abeid Amani Karume, alibaini hilo. Aliona kumbe mwenzake alikuwa na malengo yasiyokuwa ya kuungana kwa maana ya kusaidiana na kuinuana kiuchumi.
Mzee Karume ambaye alisalimisha mamlaka ya dola ya Zanzibar – Jamhuri ya Watu wa Zanzibar – alianza mapema kutoa hotuba za kumshitua Mwalimu Julius Nyerere, muasisi mwenzake wa Muungano aliyenukuliwa kabla ya hapo kuchukizwa na kuwepo kwa visiwa vya Unguja na Pemba karibu na Tanganyika.
Makubaliano ilikuwa kila mshirika wa Muungano atabaki na sheria zake kwa mambo ya maslahi ya watu wake, bunge lake, watumishi wake, mahakama yake mpaka ngazi ya Mahakama Kuu. Ushirikiano utakuja kwenye ngazi ya Mahakama ya Rufaa. Kulipaswa kuwepo Mahakama Maalum kwa ajili ya kushughulikia mizozo ya kimuungano. Haipo.
Mzee Karume aliendelea kuchukua msimamo mkali wa kuhakikisha haki za Zanzibar zinalindwa. Alithubutu kukataa maagizo mengi yaliyotoka kwa Mwalimu Nyerere, ikiwemo pale alipotumwa Waziri wa Fedha, Amir Jamal, kumshawishi aisalimishe Hazina ya Zanzibar kwa Hazina Kuu ya Tanzania. Alikataa kwa kauli kali.
Mzee Karume alisema wazi Hazina ya Zanzibar ni mali ya wananchi wa Zanzibar na akamtaka Mzee Jamal arudi na salamu hizo kwa Mwalimu Nyerere. Mpaka alipopigwa risasi tarehe 7 Aprili, 1972, Hazina ya Zanzibar ilibaki Zanzibar.
Wazanzibari wanataka nchi yenye mamlaka kamili kwa sababu wanajua wametezwa nguvu za kujiongoza kwa mambo kadhaa, yakiwemo yale yanayogusa mzizi wa uchumi. Uchumi si suala la Muungano lakini raslimali au nyezo za kuujenga, karibu zote zinadhibitiwa na Serikali ya Muungano.
Watakuzaje uchumi wao wakati hata Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ambayo katika fedha zilizotumika kuianzisha mwaka 1967, asilimia 11 ilikuwa ni mchango wa Zanzibar uliotokana na kuvunjwa kwa Bodi ya Sarafu ya Afrika Mashariki (EACB), haisimamii uchumi wa Zanzibar.
Ndio ukweli benki kuu hii kwa muda wote wa uhai wa Muungano haijishughulishi kuutizama uchumi wa Zanzibar na inapotunga sera za kifedha haijali kama zaweza kuwa na athari kwa uchumi wa Zanzibar.
Ni kwa sababu hiyo wakati fulani katika miaka ya 1990, Serikali ya Zanzibar ililalamikia hatua ya Serikali ya Muungano kuteremsha ghafla thamani ya sarafu bila ya kuifahamisha Zanzibar ambayo wakati uamuzi huo unatangazwa, ilishapanga bajeti yake.
Bajeti iliparaganyika kiasi cha kulazimu kupangwa upya. Ingetekelezwa vipi wakati ilizingatia kiwango cha thamani ya fedha ya nchi ambacho tayari kimebadilishwa? Kwa agizo la viongozi wa juu wa serikali mbili, wataalamu wa Wizara ya Fedha ya Muungano na wale wa Zanzibar walijadiliana namna ya kuipunguzia Zanzibar makali ya athari za mparaganyiko huo wa bajeti.
Na kwanini benki kuu ya Tanzania isihudumie uchumi wa Zanzibar kama inavyohudumia ule wa Tanganyika? Hizi serikali si zinatumia sarafu moja ya Shilingi? Zitatenganishwaje katika kusimamiwa kiuchumi?
Watalaamu walisema hatua hiyo ilifanywa kwa makusudi ya kuitia adabu Zanzibar kwa kuwa ilikataa kusalimisha Hazina yake. Nani asiyejua kuwa ndege mjanja hukimbiza ubawa wake? Kama wakubwa wameshaona wenzao hawakuwa na nia njema katika kutaka muungano, kwanini wasabilie kila kitu hata vile ambavyo wangenufaika vikibaki kwao tu? Ni mwendawazimu tu anayekata mkono anaolia.
Kwa miaka yote hiyo ya uhai wa Muungano, Serikali ya Muungano imeiwekea ngumu Zanzibar kutekeleza programu zake za kukuza uchumi kupitia mradi wa Bandari Huru (Duty Free Port), Maeneo Huru ya Kiuchumi (ZAFREZA). Sasa kwanini izuiwe wakati uchumi si suala la Muungano na hizo ni nyenzo za kuiwezesha kujenga uchumi wake?
Nani amesahau namna viongozi wa Zanzibar walivyodhalilishwa kwa kukaripiwa walipoingiza nchi katika Jumuiya ya Nchi za Kiislam (OIC) wakati ikijulikana wazi kilichofuatwa hapo ni fursa ya kuinua hali za wananchi kupitia misaada? Serikali ya Muungano walijua, lakini waliwalaghai Watanzania ili tu kuivunja dhamira njema ya wenzao wa Zanzibar.
Waliagiza kuitoa Zanzibar katika jumuiya hiyo kwa ahadi ya kuchukua hatua ya kujiunga. Visingizio visivyo idadi, bali hili halijatekelezwa hadi leo.
Sasa viongozi wenye upeo wa Zanzibar wameamua kushikana na Wazanzibari kudai haki ya kujiongoza. Mzee Hassan Nassor Moyo na Kamati ya Maridhiano wanaungwa mkono na umma kwa sababu wanazungumza lugha inayotii maoni ya wananchi walio wengi. Busara zao ndizo zilizosaidia kuleta utulivu uliopo baada ya kufanikiwa kushawishi viongozi wakuu wa kisiasa mwaka 2009, Amani Abeid Karume wa CCM na Maalim Seif kwa CUF na kukubaliana kufuta siasa chafu.
Kutokea viongozi wachache wakagoma kwa ghamidha na chusha, huku wakitishia wale wanaotaka mabadiliko na kuridhia mbinyo uliopo, ni kujisumbua. Utakuja wakati utashi wa Wazanzibari utakosa wa kuuzuia.
Viongozi wagumu wanachokifanya ni kuzidisha nguvu ya propaganda. Wanakaa wakitega umma unasema nini na unataka nini katika dhamira yao ya kujitawala, ndipo wajibu. Kwa bahati mbaya, wanajibu pumba si hoja zilizotolewa. Hoja hujibiwa kwa hoja zilizopangiliwa na siyo viroja.
Baada ya kuona harakati za Wazanzibari kutaka mamlaka kamili ya kujiongoza zimepamba moto, na kwa kweli haziwezi kudhoofishwa, wameamua kumbana kiongozi anayependwa na kutegemewa wakidai eti amemdharau Rais Dk. Ali Mohamed Shein aliyemteua.
Hoja ya Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai kwamba eti Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Shariff Hamad amemdharau rais kwa anachodai kutoa kauli zinazoweza kuleta mtafaruku wa maelewano kati ya Dk. Shein na Karume aliyestaafu, ni kulazimisha kosa lisilokuwepo kimantiki wala kisheria.
Anayefikiri vizuri anajua nafasi ya Karume na Maalim Seif katika hali tulivu iliyopo. Vilevile anajua nafasi ya Dk. Shein na ahadi aliyoitoa baada ya kutangazwa mshindi wa uchaguzi 2010. Je, amejiuliza kama yanayotendeka chini ya uongozi wa Dk. Shein, yote yanazingatia utashi wa wananchi walio wengi?
Je, anaweza kueleza ni nini maana ya rais kuwaambia wananchi asiokubaliana nao kimitizamo wahame nchi? Kwani alidhani urais ni kukubaliwa kila unachokiamini? Au urais ni kuamua kila unachokiwaza hata kama sivyo wananchi waonavyo? Au anaamini anayo haki ya kuongoza kwa maamuzi yoyote apendayo bila ya kuulizwa kitu na wananchi? Ndo maana akasema wananchi wanaitakia nini serikali yake, siyo?
Kama anaamini hayo, basi nahofia kuwa watu wanaongozwa kwa ulimi badala ya maarifa. Hapo kunaashiria hatari.

Anayezuia mamlaka kamili ya Zanzibar anajisumbua

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Shariff Hamad akipokea nakala ya rasimu ya Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutoka kwa Makamu wa Rais Muungano Dkt Gharib Bilal, huku Jaji Mstaafu Joseph Warioba akishuhudia
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Shariff Hamad akipokea nakala ya rasimu ya Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutoka kwa Makamu wa Rais Muungano Dkt Gharib Bilal, huku Jaji Mstaafu Joseph Warioba akishuhudia
KAMA kuna wakati ambao Wazanzibari wamepata nafasi nzuri zaidi ya kueleza hisia zao kuhusu mustakbali wa Muungano wa Tanzania, basi ni kipindi kilichoanzia tangazo la Rais Jakaya Kikwete la kuleta fursa kwa Watanzania kuandika katiba wanayoitaka.
Kwanza hiyo ni fursa ya moja kwa moja kwa mara ya kwanza kwao kujadili kwa uwazi suala hili ambalo limekuwa likiwasumbua kwa muda wote huo tangu dola yao huru ya Jamhuri ya Watu wa Zanzibar ilipounganishwa na Jamhuri ya Tanganyika Aprili 26, miaka karibu 50 iliyopita.
Ni fursa pia kwa Watanzania wa upande wa Tanganyika (nchi waliyojitia kuiita Tanzania Bara) kujadili muungano wao kwa kuwa nao, kama walivyo ndugu zao wa Zanzibar, wana maslahi makubwa kutokana na mfumo wa Muungano huo ulioasisiwa kwa nguvu kubwa na aliyekuwa kiongozi wao mkuu baada ya dola yao kupata uhuru Desemba 9 mwaka 1961, Mwalimu Julius Nyerere.
Sababu ya pili ya kujitokeza kwa fursa ya kujadili suala la muungano kwa uwazi ni ule ukweli kwamba Wazanzibari wanazo kumbukumbu nyingi za namna walivyopoteza viongozi wake wakuu kwa sababu ya hatua za viongozi hao kusimama kidete kutetea maslahi ya nchi yao, Zanzibar.
Alisumbuliwa Mzee Abeid Amani Karume kila alipotaka kubadilisha mwelekeo wa Muungano. Mzee Karume aligundua mapema sana kwamba alilaghaiwa na muasisi mwenzake wa muungano, Mwalimu Nyerere. Aligundua kuwa kumbe mwalimu hakuwa na nia njema katika kutaka Muungano.
Ndio maana Mzee Karume mara tu alipotanabahi kuwa alizungukwa, aliamua kila wakati kuchukua msimamo imara wa kuibakisha dola ya Zanzibar katika mstari wa kuwa nchi inayojitegemea. Kwa bahati mbaya, alimudu mambo machache tu lakini mengi yalimshinda kutokana na kubanwa na sheria iliyokuwepo ya mamlaka kuvikwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Wazanzibari wangali wanakumbuka kauli mbalimbali za ukakamavu alizokuwa akizitoa Mzee Karume kuonesha kupinga kuporwa mamlaka na Serikali hiyo.
Aliposema “Muungano ni kama koti likikubana livuwe,” aliposema “Muungano mwisho Chumbe,” alipofukuza mawaziri kadhaa wa Mwalimu Nyerere waliotumwa kuja kumwambia hili na lile, alipozuia safari ya wanajeshi wa Kizanzibari kwenda Msumbiji kwa kuwa hakushauriwa wala kujulishwa na muasisi mwenzake wa Muungano, Mwalimu Nyerere kuhusu safari hiyo, alikuwa anadhihirisha kupinga mfumo wa muungano.
Alipokuwa ameandaa sarafu mahsusi ya Zanzibar huku akimkatalia Waziri wa Fedha wa Mwalimu Nyerere, Mzee Amir Jamal aliyetumwa kuja kumshawishi Mzee Karume kupeleka au kusalimisha hazina yake ya fedha Tanganyika, na alipopeleka ujumbe wa kabineti yake kuwasilisha mapendekezo ya mabadiliko ya mfumo wa muungano, yote hayo ni kudhihirisha alivyopinga mapema muungano wa kinafiki.
Mapema kabisa, Mzee Karume alishuhudia namna muasisi mwenzake alivyohalifu miadi kwa kuandaa sheria zisizokubaliwa na wote wawili – badala ya zile zilizokubaliwa – ikiwemo ya kuwageuza watumishi wa Tanganyika kuwa ni watumishi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuzibadilisha sheria za Tanganyika kuwa ni sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuunda Mahakama Maalum ya Kikatiba kwa ajili ya kushughulikia mivutano ya kimuungano – na hivyo naye kuamua kwenda kulingana na matakwa ya wananchi wa Unguja na Pemba.
Mzee Karume alishuhudia vilevile, kuondolewa kwa sheria iliyoweka muda maalum wa kudumu kwa muungano huo na kutathminiwa kama una maslahi kwa washirika wake muda huo utakapokuwa umefika. Muda ulikuwa ni wa miaka 10, kwa maana ya kwamba ilikubaliwa itakapofika mwaka 1974, pande mbili zilizoungana, Tanganyika na Zanzibar, zijadili kama muungano unakidhi maslahi ya pande hizo.
Mzee Karume alipouliwa Aprili 7 mwaka 1972, miaka miwili kabla ya kufika kwa muda wa kutathmini mwenendo wa Muungano, ikaonekana kama vile ingekuwa mwisho wa harakati za Wazanzibari kudai haki ya mamlaka yao. Sivyo.
Mauaji hayo yalikuwa machungu mengine kwa Zanzibar ambayo tayari ilishashuhudia umwagikaji mkubwa wa damu ya wananchi waliodhulumiwa kwa sababu tu ya kupigania nchi yao iliyoingizwa katika muungano wa kilaghai.
Historia inaonesha viongozi wengi wa kisiasa hasa waliokuwa wasomi wa hali ya juu pamoja na maulamaa katika Uislam, waliuliwa kwa siri na kwa dhahiri kwa sababu ya misimamo yao hiyo ya kuisimamia haki ya Zanzibar na Wazanzibari.
Hapo ndipo yanakuja majina makubwa na maarufu ya kina Jaha Ubwa, Othman Sharif, Mdungi Ussi, Ibrahim Saadalla, Abdalla Kassim Hanga na wengineo waliouliwa katika matukio ya kusikitisha wengine wakiwa hawakuzikwa na jamaa zao.
Madai ya Zanzibar yaliendelezwa na Mzee Aboud Jumbe Mwinyi aliyefuata baada ya hapo, alisimama barabara kuitakia Zanzibar mamlaka yake. Kwa kuwa mfumo wa kudhoofisha yeyote ambaye angeutilia shaka muungano ulishajengwa na kuimarika kadiri siku zilivyokuwa zinakwenda, juhudi zake ziligonga mwamba.
Ilikuwa mwaka 1984 alipojikuta akihojiwa na Mwalimu Nyerere mbele ya wakuu wa vikosi vya ulinzi na usalama vya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, kwanini aliandaa waraka wa kutaka Muungano ubadilishwe ili kuirudishia Zanzibar mamlaka yake.
Ilikuwa ni bahati mbaya kwamba Mzee Jumbe aliandaa waraka wa kuitetea Zanzibar akiwa peke yake – hakumshauri au kumshirikisha yeyote kati ya mawaziri wake wakati huo. Hili ni jambo lililoleta utata mkubwa kiasi cha kusababisha mawaziri wa Serikali ya Zanzibar kumkana ilipotokea kuulizwa kama walikuwa wanajua lolote kuhusu waraka aliouandaa Mzee Jumbe.
Taarifa za ndani ya serikali zilieleza kwa umakini jambo hilo kuwa ukweli Mzee Jumbe hakushirikisha kiongozi yeyote katika kuandaa waraka huo na kwamba kwa vile wenzake hawakujua ni kitu gani hasa alichokusudia kukipata – tena labda ilikuwa ni jambo la maslahi yake binafsi kuliko nchi – wao waliona wangekumbwa wote na fagio.
Wakaukana waraka na kumtosa Mzee Jumbe. Ilikuwa ni bahati mbaya sana kwa hakika kwa sababu hata kama ilikuja kudhihirika kuwa alichokiandaa kilikuwa na maslahi makubwa ya kuikomboa nchi kutoka minyororo ya kumong’onyolewa mamlaka yake, alilenga pia kujijenga kisiasa kwa nia ya kutwaa madaraka ikitokea Mwalimu Nyerere kung’atuka.
Kilichomfika Mzee Jumbe baada ya hapo ni kulazimishwa kujiuzulu baada ya kujitetea kwa ujasiri mkubwa, huku akitaka aachiwe arudi Zanzibar ambako ndio angetangaza kujiuzulu kwa kuwa ndiko kwenye mamlaka yake. Hakuruhusiwa, badala yake alijiuzulu palepale na kuanza kutengwa kiulinzi huku akiwa amezuiliwa haki zake za kibinadamu.
Hizi ni pamoja na haki ya kuwasiliana na familia yake, haki ya kwenda atakapo, haki ya kushirikiana na watu atakao na kadhalika. Simu zilikatwa kwenye nyumba zake mbili, Unguja na Pemba.
Mzee Ali Hassan Mwinyi aliyefuata hakuwa na makubwa zaidi ya kujitahidi kuleta sera ya kuregeza masharti ya biashara hivyo kuchochea uingiaji wa bidhaa nyingi nchini zilizosaidia kuinua uchumi wa nchi na mapato ya wananchi. Alikaa kwa mwaka mmoja tu kupandishwa kwenda kuongoza Serikali ya Jamhuri ya Muungano mwaka 1985.
Katika awamu hizo mbili, Zanzibar ilianza kufunguka kidunia. Misingi ya nchi ya kidemokrasia ilianza kujengwa. Ndipo Zanzibar ikapata katiba yake huru baada ya ile iliyofutwa mara tu ilipoingia Serikali ya Mapinduzi ambapo ilipindua katiba na sheria na kuweka mahakama za wananchi badala ya zilizofuata sheria.
Paliandikwa Katiba ya 1984 ambayo ilikuwa na ruhusa ya haki zote za kibinadamu – Bill of Rights – wakati tayari likiwepo na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, mfano wa Bunge kwa nchi nyingine.
Mzee Idris Abdulwakil hakuwa na makubwa ingawa alikuwa na msimamo wa dhati wa kuitetea Zanzibar kama ilivyodhihirika wakati fulani alipoyaeleza baadhi ya mambo yanayopaswa kutizamwa upya kwa lengo la kuiwezesha Zanzibar kukuza uchumi wake.
Hapo ikaja zama ya Dk. Salimin Amour Juma ambaye alikuwa akiuma na kupuliza katika kutetea maslahi ya Zanzibar. Mara kadhaa alisikika akiwa mkakamavu lakini akisalimu amri baada ya kutishiwa na uongozi wa juu. Hili lilidhihirika alipoingiza Zanzibar katika Jumuiya ya Nchi za Kiislam – Organisation for Islamic Conference (OIC) – mwaka 1994, na kuitoa haraka baada ya Mwalimu Nyerere kutumia rungu la Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Hata hivyo, Wazanzibari hawasahau jinsi serikali yake ilivyoandaa waraka maalum wa kuyahoji masuala kadhaa yaliyo chini ya Muungano na kutaka majadiliano. Kuna tume ya Amina Salum Ali iliyokuja na mapendekezo ya kurekebisha masuala yanayoweza kuisaidia Zanzibar kiuchumi hasa kwa kuwa eneo hilo halikuwa moja na mambo ya Muungano ndio maana Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mpaka leo haitizami uchumi wa Zanzibar inapoandaa sera za kifedha.
Ila inafurahisha kukuta kwamba pamoja na hasara zote hizo zikiandamana na vitisho vya dola kubwa ya Tanganyika iliyojigeuza kinyemela na kuvaa koti la Muungano, Wazanzibari hawakutetereka. Waliendelea kudai haki yao ya kuondokana na utawala wa Waafrika wenzao.
Katika harakati zao paliandikwa vitabu na mashairi mengi kuelezea ubaya wa kuikandamiza Zanzibar. Miongoni mwa vitabu hivi ni kile alichoandika Abdulrahman Mohamed Babu kiitwacho I Saw The Future And It Works, Mzee Jumbe kiitwacho The Partnership: 30 Years of Turbulent Zanzibar na Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru alichoandika Dk. Harith Ghassany, Mzanzibari aliyelewea Uarabuni.
Hatua za sasa ni mfululizo wa jitihada za Wazanzibari kudai haki ya kurudisha mamlaka yao ya kujitawala. Kama si sasa basi hakika ni halafu hakutakuwa na namna ya kuzuia madai yao. Italazimu haki iachiwe kusimama.
Chanzo: Fahamu – Kalamu ya Mzanzibari