Monday, July 15, 2013

Katiba Mpya iondoe vikwazo vya rasilimali za nchi – Maalim Seif


Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad akisalimiana na Naibu Waziri wa Uingereza anayehusika na Mambo ya Nje na Jumuiya ya Madola, Mark Simmonds, alipofika nyumbani kwake Mbweni pamoja na ujumbe wake kwa mazungumzo.
Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad akisalimiana na Naibu Waziri wa Uingereza anayehusika na Mambo ya Nje na Jumuiya ya Madola, Mark Simmonds, alipofika nyumbani kwake Mbweni pamoja na ujumbe wake kwa mazungumzo.
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad amesema matarajio ya wananchi kuhusu mchakato wa mabadiliko ya katiba ni kuona unaondoa vikwazo vya utafutaji na matumizi ya rasilimali asili zikiwemo mafuta na gesi.
Maalim Seif ameeleza hayo nyumbani kwake mbweni alipokuwa na mazungumzo na ujumbe wa Uingereza ulioongozwa na Naibu Waziri anayehusika na Mambo ya Nje na Jumuiya ya Madola, Mark Simmonds ambapo pamoja na mambo mengine walizungumzi juu  mchakato wa katiba na maendeleo ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia Zanzibar.
Amesema wakati Zanzibar imeshaamua kuliondoa suala hilo katika orodha ya mambo ya Muungano, bado inasubiri taratibu za kisheria ambazo zinaweza kupatikana baada ya kukamilika kwa mchakato wa katiba.
Amesema mara baada ya kukamilika kwa mchakato huo na suala la mafuta na gesi asilia kuondolewa katika mambo ya Muungano, Zanzibar itatangaza zabuni za uchimbaji wa mafuta na gesi asilia ambapo makampuni mbali mbali yataruhusiwa kuomba zabuni hizo, na hatimaye kuanza rasmi kwa kazi ya uchimbaji.
Amefahamisha kuwa mchakato wa katiba umefikia hatua nzuri baada ya kuanza kwa mabaraza ya katiba tarehe 12/07/2013, ambayo itafuatiwa na bunge la katiba na baadaye wananchi wataamua katiba hiyo kupitia kura ya maoni.
Kuhusu nishati ya umeme ambapo Uingereza ni mshirika wa karibu wa nishati hiyo nchini, Maalim Seif amesema Zanzibar imo katika mchakato wa kutafuta nishati mbadala itokanayo na jua pamoja na upepo, ambapo tayari imeonesha mwelekeo mzuri.
Amesema nishati hiyo itakapopatikana itaondosha usumbufu unaojitokeza mara kwa mara na kupunguza utegemezi wa upatikanaji wa umeme kutoka Tanzania Bara, sambamba na kupunguza uchafuzi wa mazingira.
Aidha Maalim Seif ameelezea mazingira ya uwekezaji Zanzibar, na kuuomba ujumbe huo kuhamasisha wawekezaji kuja kuwekeza hasa katika sekta za utalii na uvuvi wa bahari kuu.
Amesema Zanzibar ambayo kwa sasa imetoa kipaumbelele katika sekta ya utalii, inakaribisha wawekezaji katika ujenzi wa hoteli za nyota tano katika visiwa vya Unguja na Pemba.
Ameongeza kuwa Zanzibar pia ina mpango wa kujenga bandari ya kibiashara katika eneo la mpigaduni, pamoja kuvifanyia matengenezo makubwa viwanja vya ndege, ili kuweka mazingira bora zaidi ya uwekezaji.
Naye Bwana Simmonds amesema Uingereza itaendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta mbali mbali ikiwemo nishati.
Ameahidi kuwasiliana na makampuni ya utalii, uvuvi na ujenzi ili kuangalia uwezekeno wa kuja kuwekeza Zanzibar katika maeneo mbali mbali nchini.

Bei za vyakula afadhali kidogo – Maalim Seif

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad akihoji bei ya samaki aina ya change katika soko la Darajani, wakati wa ziara yake ya kutembelea soko hilo. Changu mmoja wa kawaida anauzwa kwa bei ya shilingi 8000 hadi 10,000.
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad akihoji bei ya samaki aina ya change katika soko la Darajani, wakati wa ziara yake ya kutembelea soko hilo. Changu mmoja wa kawaida anauzwa kwa bei ya shilingi 8000 hadi 10,000.
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad ameelezea kuridhishwa kwake na uwepo wa bidhaa muhimu pamoja na matunda katika masoko mbali mbali ya Zanzibar.
Amesema bei ya bidhaa nyingi inaridhisha tofauti na ilivyokuwa Ramadhani ya mwaka jana, lakini tatizo kubwa ni hali ngumu ya uchumi kwa wananchi.
Maalim Seif ametoa kauli hiyo wakati wa ziara yake ya kutembelea masoko ya bidhaa na matunda katika manispaa ya Zanzibar.
Masoko aliyoyatembelea ni pamoja na soko la Mombasa, Mwanakwerekwe na soko kuu la Darajani.
Katika ziara hiyo ambayo aliambatana na Waziri wa Biashara Nassor Mazrui, Waziri wa Nchi na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mwinyihaji Makame pamoja na viongozi wa Mkoa na Manispaa, Maalim Seif alijionea hali halisi ilivyo katika masoko hayo.
Miongoni mwa bidhaa muhimu alizozihoji ni pamoja muhogo, ndizi mbichi na mbivu, majimbi, maboga, matunda mbali mbali, nyama na samaki.
Amesema kwa ujumla ameridhishwa na uwepo wa bidhaa hizo kwa wingi, licha ya bei ya baadhi ya bidhaa hizo kuwa juu na kupelekea wananchi kutumudu kununua.
Hata hivyo ameelezea kusikitishwa kwake na bei kubwa ya vitoweo, na kuwataka wachuuzi kufikiria namna ya kuwasaidia wananchi wa kawaida.
Ameitaka Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais kusimamia utaratibu ulioweka wa kuweko minada katika soko la Mombasa, ili kuondosha usumbufu na msongomano katika masoko mengine.
Akizungumza na wafanyabiashara wa jua kali, Maalim Seif amesema serikali haipendi kuona wananchi wananyanyasika, na kutaka pawepo utaratibu mzuri wa kuendesha biashara katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Hata hivyo amewataka wafanyabishara hao kufuata utaratibu watakaowekewa na mamlaka zinazohusika ikiwa ni pamoja na kutoweka biashara njiani zinazopelekea kufunga njia na kuleta usumbufu wa wateja na wananchi kwa jumla.
Amesema baada ya mwezi mtukufu wa Ramadhani kumalizika, wafanyabiashara hao watapangiwa utaratibu wa kurejea katika soko la Saateni ambako kituo kikuu cha magari pia kitahamishiwa eneo hilo.
Mapema wafanyabiashara hao waliomba waruhusiwe kufanya biashara katika mwezi huu wa Ramadhan na kuahidi kuondoka baadha ramadhani kumalizika.
Nao wafanyabiashara wa masoko hayo wameelezea juu ya kadhia wanazokumbana nazo zikiwemo uvamizi unaofanywa na baadhi ya wafanyabiashara wadogo wadogo nje ya masoko, hali inayopelekea ugumu wa biashara katika maeneo ya ndani ambayo wamekuwa wakilipia kodi.
Nae Mkurugenzi wa Baraza la Manispaa Zanzibar Abeid Juma, amesema wamekuwa wakizungumza na wafanyabiashara mara kwa mara juu ya utaratibu wa kuendesha biashara zao, lakini bado wafanyabiashara hawajajipanga vizuri kukubaliana na taratibu hizo.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Mwinyihaji Makame, kwa upande wake ameahidi kukutana na wafanyabiashara wa soko la darajani ili kujadiliana juu ya utaratibu bora wa kuendesha biashara katika soko hilo.
Chanzo: Ofisi ya Makamao wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar