Saturday, July 20, 2013

Hotuba ya kwanza ya rais Adly Misri


Chama cha Muslim Brotherhood nchini Misri kimetoa wito kwa mamilioni ya watu kushiriki maandamano mengine dhidi ya hatua ya jeshi la nchi hiyo kumpindua kiongozi aliyechaguliwa Mohamed Morsi.
Katika taarifa yake, kiongozi wa Muslim Brotherhood Mohamed Badie, ametoa wito kwa jeshi kufikiria upya hatua yake na likubali wanachotaka watu.
Lakini katika hotuba yake ya kwanza tangu kuwa kaimu rais, Adly Mansour, ameahidi kuimarisha usalama na utulivu dhidi ya wale wanaotaka kuzusha ghasia nchini Misri
Wiki mbili baada ya jeshi kumwondoa mamlakani Mohammed Morsi, bwana Mansour alisema kuwa serikali yake itajitolea kuhakikisha kuna usalama na uthabiti.
Wakati huohuo, chama cha Muslim Brotherhood kimekataa kujiunga na baraza la muda la mawaziri lililotangazwa wiki hii.
"tunapitia kipindi kigumu, na baadhi wanataka vurugu ilihali tunataka kusonga mbele,'' alisema kaimu kiongozi wakati akitoa hotuba kwenye televisheni.
"tutapigana vita vya kuhakikisha kuna usalama na tutalinda mapinduzi.''
Bwana Morsi aliondolewa mamlakani tarehe tatu mwezi Julai katika kile wafuasi wake walisema ni mapinduzi ya kijeshi.
Jeshi hata hivyo linasema kuwa lilikuwa linatimiza mahitaji ya watu baada ya mapinduzi ya kijeshi.

Nigeria kuondoa wanajeshi wake Mali


Jeshi la Nigeria
Nigeria inapanga kuondoa baadhi ya wanajeshi wake, kati ya 1,200 kutoka jeshi la kulinda amani la Umoja wa Mataifa nchini Mali, Rais wa Ivory Coast Alassane Ouattara ametangaza.
Rais Ouattara ambaye ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Uchumi ya Nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS, amesema wanajeshi hao wanahitajika nyumbani kukabiliana na wanamgambo wa Kiislam.
Haijafahamika bado ni vikosi vingapi vya Nigeria vitabakia Mali, ambako uchaguzi mkuu unatarajiwa kufanyika tarehe 28 Julai.
Wanajeshi wa Nigeria ni sehemu ya jeshi la Afrika lenye askari 12,600 ambao walichukua jukumu la kulinda amani kutoka kwa Ufaransa Julai mosi mwaka huu.
Vikosi vya Ufaransa na Afrika viliwatimua wanamgambo wa Kiislam kutoka kaskazini mwa Mali Februari mwaka huu.
Jeshi la Umoja wa Mataifa sasa linashirikiana na jeshi la Mali kulinda usalama kwa ajili ya uchaguzi. Linatarajiwa kuongezeka hadi kufikia askari 11,200, pamoja na polisi 1,400 ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.
Akizungumza kwenye mkutano wa viongozi wa mataifa ya Afrika Magharibi, katika mji mkuu wa Nigeria, Abuja, Rais Ouattara amesema kuondolewa kwa wanajeshi hao kunatokana na matatizo ya ndani nchini Nigeria.
“Hawataondoa wanajeshi wote. Sehemu muhimu ya vikosi hivyo itabakia Mali,” amesema.
Zaidi ya watu 2,000 wameuawa tangu wanamgambo wa Kiislam wa kundi la Boko Haram walipoanzisha uasi mwaka 2009 ili kuunda taifa la Kiislam katika eneo lenye Waislam wengi la Kaskazini mwa Nigeria.
Hali ya hatari ilitangazwa tarehe 14 Mei katika majimbo ya kaskazini mashariki ya Adamawa, Borno na Yobe, huku zaidi ya wanajeshi 2,000 wakipelekwa kuvunja kambi za Boko Haram na operesheni za uasi.
Uchaguzi mkuu wa mwezi huu nchini Mali una lengo la kumaliza miezi ya mtafaruku wa kisiasa ulioanza baada ya wanajeshi kumpindua Rais Amadou Toumani Toure mnamo Machi 2012, na kuruhusu waasi na wanamgambo wa Kiislam kudhibiti eneo la kaskazini mwa nchi hiyo.
Ufaransa ambayo ilikuwa mkoloni wa zamani wa mali ilipeleka zaidi ya askari 4,000 Januari mwaka huu baada ya waasi kutishia kuuteka mji mkuu wa Mali, Bamako.
Nchi za Magharibi zimeahidi kutoa msaada wa dola za Kimarekani bilioni 43 kusaidia kufufua uchumi wa Mali, ukiwa unahusishwa na utekelezaji wa mpango wa maridhiano ya kisiasa na kufanyika kwa uchaguzi mkuu.

Mateka wa MSF waachiliwa na Al shabaab


Montserrat Serra (kushoto) na Blanca Thiebaut (Kulia) walipelekwa Somalia na watekaji wao

Wahudumu wawili wa shirika la madaktari wasio na mipaka - MSF wameachiliwa huru na wapiganaji wa Al Shabaab.Wahudumu hao walitekwa nyara mwaka 2011 katika kambi ya wakimbizi wa Kisomali kaskazini mwa Kenya.
Shirika la Medecins Sans Frontieres limesema kuwa wafanyakazi hao wawili wote wako salama na wenye afya na wanatazamia sana kujiunga na jamaa zao.
Montserrat Serra na Blanca Thiebaut walitekwa nyara kutoka kambi ya wakimbizi ya Dadaab mwezi Oktoba mwaka 2011.
Kufuatia kutekwa nyara kwao pamoja na mateka wengine wa Kenya, nchi hiyo ililazimika kutuma vikosi nchini Somalia kupambana na wanamgambo wa al-shabaab.
Katika taarifa ya shirika hilo, ni afueni kubwa kwa shirika hilo kuweza kuthibitisha kuachiliwa kwa wanawake hao.
Wanawake hao walitekwa nyara tarehe 13 mwezi Oktoba mwaka 2011 na watu waliokuwa wamejihami kwa bunduki na ambao walifyatulia risasi gari la wanawake hao huku wakimjeruhi dereva aliyekuwa raia wa Kenya.
Kambi hiyo ya Dadaab ambayo ndiyo kambi kubwa zaidi duniani ya wakimbizi, inawahifadhi wakimbizi laki tano ambao wametoroka vita vya miaka mingi na njaa nchini Somalia ambayo inapakana na Somalia.
Bi Serra, ambaye ni mwalimu kutoka , Girona nchini uhispania, alikuwa mfanyakazi nchini Kenya kwa miezi miwili alipotekwa nyara. Alikuwa amefanya kazi na mashirika mengione ya misaada Amerika ya kusini na Yemen.
Moja ya magari yaliyotumiwa kuwateka nyara wafanyakazi hao

Mwanamke mwingine Thiebaut ambaye ni mhandisi wa kilimo, kutoka Madrid alikuwa ndio amekamilisha tu masomo yake ya digri katika chuo cha mafunzo ya uchumi mjini London alipotekwa nyara.
Kenya ililituhumu kundi la al-Shabab kwa kuhusika na utekaji nyara huo pamoja na matukio mengine sawa na hilo mwaka 2011 na hivyo kutishia usalama wa nchi.
Ilituma vikosi vyake nchini Somalia kuweza kupambana nao na kisha kuteka maeneo mengi ya nchi hiyo kutoka kwa kundi la al-Shabab.
Wanajeshi wake nchini Somalia sasa wamejiunga na kikosi cha jeshi katika muungano wa Afrika ambao wanasaidia serikali dhaifu ya Somalia.

Askari akamatwa kwa kudhalilisha maiti



Wanajeshi wa DRC wakitoa ulinzi katika eneo la Kanyarucinya, yapata kilomita 12 kutoka mji wa Goma.
Afisa mmoja wa jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ametiwa nguvuni baada ya kuchafua maiti za wapiganaji wa waasi nchini humo.
Waziri wa mashauri ya nchi za kigeni wa DRC, Lambert Mende, ameiambia BBC kwamba Luteni Solomo Bangala alizuiliwa jana Alhamisi na maafisa wa kijeshi baada ya mapigano kuzuka kati ya jeshi na waasi wa M23 katika eneo la mashariki karibu na mji wa Goma.
Kukamatwa kwa afisa huyo kunajiri muda mfupi tu baada ya katibu mkuu wa umoja wa mataifa Ban Ki Moon kuzungumzia madai ya kuwepo dhuluma na mateso dhidi ya wafungwa kutoka makundi ya waasi pamoja na wale waliouwawa zinazotekelezwa na wanajeshi wa Kikongomani.
Kikosi cha kulinda amani cha umoja wa mataifa kinatathmini upya hatua yake ya kuunga mkono vikosi vya serikali ya DRC kufuatia shutuma hizo.

Waasi wa M23
Mapigano kati ya jeshi la DRC na waasi wa M23 yalianza siku ya Jumapili karibu na mji wa Goma.
Mwandishi wa BBC Maud Jullien aliyepo katika mji wa Goma anasema uwanja wa mapigano ulikuwa takriban kilomita 7 katika vilima kutoka mji huo.
Hapajakuwa na mapigano yoyote katika kipindi cha siku mbili zilizopita na jeshi limesema limefanikiwa kuwafukuza waasi yapata kilomita 6, anasema mwandishi wetu.
Mwezi Novemba, wanamgambo wa M23 waliuteka kwa kipindi kifupi mji wa Goma, kisha wakaondoka baada ya kutimizia msururu wa ahadi ikiwemo kuanzisha mazungumzo na serikali.
Waasi wa M23, ambao kwa wingi wanatoka kabila la Watutsi walijiondoa katika jeshi la serikali mwezi Aprili mwaka 2012, na kuanzisha mapigano yaliyowaacha takrikaban watu 800,000 bila makao katika eneo hilo lenye utajiri mkubwa wa madini.
Mazungumzo ya amani yaliyofanyika nchini Uganda mwaka huu ili kushughulikia malalamishi ya waasi hao yamekwama.