Thursday, June 6, 2013

Watoto Finland hulazwa kwa visanduku vya Karatasi?

Kwa miaka 75, kina mama wajawazito wamekuwa wakipewa na serikali visanduku vya karatasi. Visanduku hivyo vimekuwa vikitolewa kama sehemu ya vitu muhimu vya mwanzo kwa mtoto atakapozaliwa, kama vile vile nguo, mashuka na midori, ambavyo pia vinaweza kutumika kama kitanda. Na baadhi ya watu wanasema vitu hivyo vimeisaidia Finland kufanikiwa kuwa moja ya nchi ambayo ina viwango vya chini kabisa vya vifo vya watoto duniani.
Imekuwa ni desturi iliyojengekea ambapo visanduku vya karatasi hutolewa kwa mama wajawazito tangu miaka ya 1930 na imepangwa na serikali kutolewa kwa watoto wote nchini Finland, bila kujali hali ya familia wanazotoka, ni mwanzo wenye usawa katika maisha ya watoto.
Vifaa vya uzazi - ni zawadi kutoka serikalini na ipo kwa mama wote wajawazito.
Vifaa hivyo ni pamoja na nguo za mtoto, mfuko wa kulalia, vifaa vya kumbebea nje ya nyumba, sabuni za kuogea na mafuta ya mtoto, pamoja na nepi, matandiko na godoro dogo.
Godoro likiwa ndani ya kisanduku cha karatasi linakuwa kitanda cha kwanza cha mtoto. Watoto wengi kutoka familia zenye hali tofauti za maisha, kwanza wanalala katika sanduku salama la karatasi la pembe nne.
Mpango wa mwaka 1947 wa vifaa kwa mama mzazi, unampa chaguo la kuchukua sanduku hilo au kuchukua ruzuku ya fedha taslimu, ambayo kwa sasa ni euro 140, lakini asilimia 95% wanapendelea kuchukua sanduku ambalo lina thamani zaidi.
Utamaduni huuu umedumu tangu mwaka 1938. Kwa kuanzia, mpango huu uliwahusu tu familia zenye vipato vya chini, lakini ukabadilika mwaka 1949.
"Si tu kwamba uliwalenga wanawake wanaotarajia kujifungua lakini sheria mpya ilimaanisha, ili kupata ruzuku hiyo, au sanduku la mzazi, walitakiwa kumwona daktari au muuguzi wa zahanati ya manispaa kabla ya kufikisha miezi minne ya ujauzito," anasema Heidi Liesivesi, ambaye anafanya kazi Kela - Taasisi ya Bima ya Jamii ya Finland.
Kwa hiyo sanduku hilo linakuwa na vitu muhimu ambavyo mama wazazi wanatakiwa kuwa navyo kwa ajili ya watoto wao wachanga, lakini pia inasaidia wanawake wajawazito kuwa katika uangalizi wa madaktari na wauguzi wa serikali ya Finland.
Katika miaka ya 1930 Finland ilikuwa nchi maskini na kiwango cha vifo vya watoto kilikuwa cha juu ambapo katika kila watoto 1,000 waliozaliwa, 65 walifariki dunia. Lakini hali hiyo ilibadilika haraka katika miongo iliyofuata.
Mika Gissler, profesa katika Taasisi ya Taifa ya Afya na Ustawi mjini Helsinki, anatoa sababu kadha kuhusu hili- sanduku la uzazi na huduma za kabla ya uzazi kwa wanawake katika miaka ya 1940, ikifuatiwa na mfumo wa Bima ya Afya ya Taifa katika miaka ya 1960 na mtandao wa hospitali kuu.

Wachina wakamatwa Ghana kwa uchimbaji haramu


Ghana huzalisha kiwango kikubwa zaidi cha dhahabu barani Afrika
`Maafisa wa uhamiaji nchini Ghana wanasema kuwa polisi wamewakamata zaidi ya raia 150 wa uchina ambao wanashukiwa kuhusika na uchimbaji wa dhahabu kinyume na sheria.
Kulingana na Francis Palmdeti kutoka idara ya uhamiaji nchini Ghana,raia hao wanazuiliwa katika migodi minne tofauti nchini humo.
Mamlaka nchini Ghana ilikuwa imewataka raia wote wa kigeni kutohusika katika uchimbaji madini.
Taarifa zinasema kuwa raia wengi wa uchina wamekuwa wakihusishwa na uchimbaji madini wa kiwango cha chini nchini humo baada ya kuingia kinyume cha sheria kupitia mataifa jirani.
Hata hivyo msemaji wa ubalozi wa uchina nchini Ghana anasema kwamba anataraji kuwa raia hao watarudishwa makwao.
Wakati huohuo, wizara ya mambo ya kigeni ya Uchina imelalamikia serikali ya Ghana baada ya wafanyakazi hao wa China kuzuiliwa kufuatia msako uliofanywa wa wachimbaji haramu wa madini.
Ghana ndiyo nchi yenye kuzalisha kiwango kikubwa cha Dhahabu baada ya Afrika Kusini barani Afrika.
Huku bei ya dhahabu ikiendelea kupanda katika miaka ya hivi karibuni, sekta hiyo imekuwa ikikumbwa na wachimbaji haramu wa madini hayo ikiwemo, idadi kubwa ya wafanyakazi wa kichina inayoendelea kuongezeka.
China imesema kuwa intaka watu hao kutoteswa na kutoibiwa wakati wa msako huo.

Vijusi wanaweza kuonyesha hisia tumboni

Vijusi wakijifunza kuonyesha hisia za uchungu wakiwa bado tumboni
Vijusi au mtoto ambaye angali kuzaliwa akiwa bado kwenye mfuko wa uzazi, hujifunza kuonyesha hisia za uchungu wakiwa bado tumboni. Hii ni kwa mujibu wa utafiti uliofanywa katika vyo vikuu vya Durham na Lancaster nchini Uingereza.
Wanaamini kuwa vijusi hujifunza namna ya kuwasiliana baada ya kuzaliwa kwa njia za kulia au kwa kukunja uso wakiwa tumboni.
Utafiti huo uliofanywa kwa kupiga picha za Ultrasound, ulionyesha kuwa vijusi hujifunza kusonga na kuonyesha hisia wakati wakiwa tumboni.
Picha hizo zilionyesha hisia za vijusi hao wakati wa ujauzito wakionekana wakicheka, au kutabasamu, kukunja uso na hata kuvuta pua.
Mtafiti mkuu Daktatri Nadja Reissland, alisema kuelewa namna ambavyo mtoto anakuwa tumboni, inaweza kuwasaidia madaktari kujua ikiwa kuna matatizo yoyote na watoto kabla ya kuzaliwa.
"haijulikani ikiwa vijusi wanaweza kuhisi uchungu au haijulikani ikiwa kwa kukunja uso ni ishara tosha kuonyesha ikiwa vijusi wanahisi uchungu,'' alisema daktari huyo.
Utafiti ulionyesha kuwa mkunjo wa uso ni dalili ya ubongo kukuwa kuliko kuonyesha hisia za uchungu.
Utafiti ulitumia kanda ya video iliyokuwa na picha tatu za Ultrasound za vijusi wanane wasichana na saba wavulana.
Utafiti huu unakuja baada ya utafiti uliofanywa hapo awali ukipendekeza kuwa vijusi wenye afya nzuri huendelea kukuwa wakati ujauzito ukiendelea kukoma.
Daktari Reissland, mtafiti mkuu katika chuo kikuu cha Durham, amesema kuwa ni muhimu kwa vijusi kuonyesha hisia za uchungu mara wanapozaliwa ili waweze kuonyesha ikiwa wana uchungu huku wakirahisisha mawasiliano na wazazi wao.

Paris Jackson ajaribu kujiua

 

Wanawe marehemu Jackson, Paris,Prince na Blanket
Bintiye marehemu Michael Jackson, Paris, mwenye unmri wa miaka 15, amelazwa katika hospitali moja mjini Carlifornia baada ya kujaribu kujiua. Msemaji wa familia ameeleza kuwa anaendelea kupata nafuu na kuwa madaktari wanamshughulikia vilivyo.
Inasemekana, Paris Jackson, ambaye babake alifariki mwaka 2009, amekuwa katika hali ya kusononeka kwa muda sasa.
Msemaji wa familia hiyo amesema kuwa usiku wa kuamkia jana binti huyo alikimbizwa hospitalini baada ya kujaribu kujiua lakini anaendelea kupata nafuu.
Msemaji alifafanua kuwa hali yake si mbaya sana ya kupelekwa kwa wadi ya wagonjwa mahututi.
Paris Jackson ametajwa kama mmoja wa familia ya Michael Jackson anayetaka kulipwa mamilioni ya Dolar kutoka kampuni ya AEG ambayo ilimwajiri daktari aliyempa madawa Michael ambayo yaligunduliwa baadaye kuwa yalimwua.
Kesi inayohusiana na madai hayo imeendelea kwa majuma sita sasa. Mengi ya kusikitisha juu ya Michael Jackson yamekuwa yakitajwa na inadhaniwa kwamba yamechangia pakubwa kupandisha huzuni na simanzi kwa msichana Paris.
Inadhaniwa kuwa Paris amejaribu kadiri ya uwezo wake kumwomboleza baba yake lakini angali anasononeka kutokuwepo kwake. Mlezi wake kisheria ni nyanya yake Catherine lakini hata hivyo siku chache zilizopita amekuwa akiishi na mamake mzazi.

Uingereza yakubali kuwafidia Mau Mau


 7 Juni, 2013 

Uingereza imekubali kuwalipa fidia na kuwaomba msahama walioteswa wakati wa ukoloni wa Muingereza Kenya
Serikali ya Uingereza imetangaza kuwa itawalipa fidia ya dola milioni thelathini manusura wa harakati za ukombozi wa Uhuru wa Kenya Mau Mau.
Waziri wa mambo ya nje wa Uingereza William Hague ametangaza kuwa serikali yake itawalipa wale wote walioteswa na askari wa ukoloni katika miaka ya 1950.
Waliokuwa wanachama wa vuguvugu hilo waliwasilisha kesi mahakamani kwa mateso na dhuluma walizodai kutendewa na uliokuwa utawala wa ukoloni miaka ya 50.Huenda pia Uingereza itatangaza fidia.
Waliokuwa wanachama wa vuguvugu hilo waliwasilisha kesi mahakamani kwa mateso na dhuluma walizodai kutendewa na uliokuwa utawala wa ukoloni miaka ya 50.Huenda pia Uingereza itatangaza fidia.
Zaidi ya wakenya 5,000, waliteswa baadhi wakinyanyaswa na waliokuwa wakoloni wa Uingereza.
Uingereza ilipigana vita vikali dhidi ya Mau Mau, waliokuwa wanadai ardhi na kuondoka kwa utawala wa kikoloni.
Baadhi ya waliokuwa wanachama wa Mau Mau
Manusura wa vita hivyo wamekuwa wakiidai Uingereza kuwalipa fidia kwa miaka mingi.
BBC ina habari kuwa bwana Hague atawaomba radhi waathiriwa wa vita vya Mau Mau, wakati akitangaza kiwango cha pesa watakazotoa kama fidia kwao.
Serikali ya Uingereza awali ilikuwa imesema kuwa madai yote ya vitedno walivyofanya wakoloni ni juu ya serikali ya Kenya tangu kuipa uhuru mwaka 1963 na kuwa kwa sasa haiwezi kutakiwa kulipa.
Lakini mwaka 2011, mahakama iliamuru kuwa, wanaodai fidia, Paulo Muoka Nzili, Wambuga Wa Nyingi na Jane Muthoni Mara, walikuwa na haki ya kudai fidia kutoka kwa Uingereza .
Mawakili wao wanasema kuwa Nzili alihasiwa , huku Bwana Nyingi akichapwa vibaya wakati Bi Mara akiteswa kimapenzi katika kambi za mateso ambako waliokuwa wanapinga ukoloni walikuwa wakifungwa.
Baada ya uamuzi wa kesi hiyo, ilirejeshwa katika mahakama kuu ili kuamua pesa watakazolipwa na ofisi ya jumuiya ya madola.
Mahakam kuu Uingereza iliamua kuwa walalmishi walipaswa kutendwa haki
Duru zinasema kuwa serikali ilikumbwa na wakati mgumu kupata mashahidi na stakabadhi muhimu kuweza kuelezea ukweli katika kesi hiyo.
Lakini Oktoba mwaka jana, mahakama iliamua kuwa waathiriwa waliowasilisha kesi hiyo mahakamani walikuwa na haki ya kufidiwa kwani walikuwa na kesi nzito dhidi ya serikali ya Uingereza.
Watatu hao walikuwa wamesema kuwa wangekubali wahusika wa kesi kuafikiana nje ya mahakama lakini pia walikuwa wanataka kufuata sheria kwani waliona wangepata haki katika mahakama.