Friday, May 3, 2013

Serikali kukaza uzi timuatimua wanafunzi wakorofi vyuo vikuu


Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imesisitiza kuwa itaendeleza utaratibu wa kuwafukuza wanafunzi wa vyuo vikuu ambao watakuwa na tabia za utovu wa nidhamu na migomo isiyokuwa na lazima.
SHARE THIS STORY
Dodoma. Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imesisitiza kuwa itaendeleza utaratibu wa kuwafukuza wanafunzi wa vyuo vikuu ambao watakuwa na tabia za utovu wa nidhamu na migomo isiyokuwa na lazima.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philip Mulugo.
Alisema Serikali haina kigugumizi cha kuona ni kwa nini isiwafukuze wanafunzi wa aina hiyo ambao wanakuwa ni kichocheo cha migogoro.
Alitoa kauli hiyo wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema), ambaye alitaka kujua mkakati wa Serikali kuwarudisha wanafunzi wa vyuo vikuu ambao walifukuzwa masomo yao kutokana na migogoro iliyoibuliwa vyuoni mwao.
Katika swali la msingi Mnyika alitaka kujua hatua za Serikali katika kuwarudisha wanafunzi hao kutoka vyuo vya Dodoma (Udom), Dar es Salaam na Chuo Kikuu Kishiriki cha Sayansi (MUHAS).
Mbali na hilo, aliomba ripoti ya Tume ya Rais iliyoundwa mwaka 2011 kwa ajili ya kuangalia migogoro hiyo kwa wanafunzi ambayo imedumu kwa muda mrefu ili ipelekwe bungeni na kujadiliwa kabla ya kumshauri Rais jambo la kufanya.
Naibu Waziri alisema katika migogoro hiyo, kuna maeneo ambayo wanafunzi walisimamishwa masomo na baadhi walirudishwa masomoni, lakini wengine bado hawajarudishwa.
“Mfano, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, wanafunzi waliosimamishwa ni 99, lakini 78 walirudishwa na 21 hawajarudishwa, kwa Udom walisimamishwa 570 lakini 563 walirudishwa masomoni na 7 wamefukuzwa kabisa, kingine ni MUHAS ambapo walisimamishwa wanafunzi 115 wengine wamerudi na wengine watarudi Desemba mwaka huu wakati wanafunzi wawili wamefukuzwa kabisa,” alisema Mulugo.
Kuhusu ripoti ya Rais, Mulugo alisema ilikuwa ni tume maalumu kwa ajili ya kumsaidia Rais, hivyo siyo lazima ripoti yake kupelekwa bungeni kama ambavyo wabunge wanataka.

MFANYABIASHARA KARIAKOO AJIRUSHA TOKA GHOROFA YA TISA NA KUANGUKIA GARI MCHANA HUU

Muda mfupi uliopita,Mtu mmoja alietambulika kwa jina la Shirima ambaye ni Mfanyabiashara katika moja ya Maduka ya Kariakoo jijini Dar es Salaam,amejirusha toka ghorofa ya 9 ya Hoteli ya Concord iliopo Maeneo ya Kariakoo jijini Dar es Salaam na amekimbizwa hospitali kwa uangalizi zaidi maana haijafahamika kama kapoteza Maisha au bado yu hai.

Mfanyabiashara huyo alijirusha toka ghorofani na kuangukia Gari aina ya Toyota Corolla ambayo ni taxi iliyokuwa imepaki nje ya hoteli hiyo....chanzo cha kujirusha kwa mfanyabiashara huyo bado hakijafahamika mpaka sasa.

Mashuhuda wa tukio hilo lililotokea muda mfupi uliopita,wanaeleza kuwa walipatwa na mshuko baada ya kusikika kishindo cha kitu kilichokuwa kimeangukia gari hilo na waliposogea kushuhudia ndipo walipobaini kuwa alikuwa ni mtu huyo alietambulika kwa jina moja la Shirima.

Njama ya mapinduzi yatibuliwa Chad

 2 Mei, 2013 

Watu kadhaa akiwemo mbunge wa upinzani wamekamatwa katika mji mkuu wa Chad Ndjamena, katika kile ambacho serikali inasema ilikuwa njama ya kuvuruga hali nchini humo.
Taarifa kutoka kwa vyombo vya serikali zinasema kuwa kundi moja dogo la watu limekuwa likipanga njama hiyo kwa miezi minne.
Viongozi wa njama hiyo ya mapinduzi wanachunguzwa na viongozi wa mashtaka.
Chad ina historia ndefu ya mapinduzi na uasi. Rais wa sasa Idriss Deby mwenyewe alichukua mamlaka kwa njia ya mapinduzi mwaka 1990.
Serikali ilisema kuwa kundi moja la watu wenye nia mbaya walijaribu kufanya mapinduzi dhidi ya taasisi za nchi.
Ilisema kuwa maafisa wa usalama wa serikali walikabiliana nao bila kutaja idadi yao.
Polisi pamoja na duru za upinzani zilisema kuwa mbunge huyo Saleh Makki alikuwa miongoni mwa waliokamatwa.
Pamoja na waliokamatwa ni wanajeshi kadhaa
Tangu nchi hiyo kujipatia uhuru kutoka kwa Ufaransa, mwaka 1960, Chad imekumbwa na misukosuko hasa kati ya eneo la Kaskazini ambalo lina waarabu wengi na Kusini ambako kuna wakristo wengi.
Mapema mwaka huu Chad iliwapeleka wanajeshi 2,000 kujaribu, kuwatimua wapiganaji walioteka sehemu kubwa ya Mali.

60,000 walikufa wakati wa ukame Somalia

 2 Mei, 2013 


Watoto wengi walikufa kutokana na utapia mlo
Takriban watu 260,000 walifariki dunia wakati wa ukame ulioikumba Somalia kuanzia mwaka 2010 hadi 2012, utafiti umebaini.
Nusu ya waliofariki dunia walikuwa ni watoto wenye umri chini ya miaka mitano, inaeleza ripoti ya shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo, FAO, pamoja Mtandao wa Kuonya Mapema Kuhusu Majanga ya Ukame unaofadhiliwa na Marekani.
Idadi ya vifo ilikuwa kubwa kuliko ile iliyokadiriwa ya watu 220,000 waliofariki wakati wa ukame wa mwaka 1992.
Janga hilo lilisababishwa na ukame mkali, uliochochewa na mapigano kati ya makundi hasimu yaliyokuwa yakigombea madaraka.
Umoja wa Mataifa kwa mara ya kwanza ulitangaza hali ya ukame Julai 2011 katika mikoa ya Somalia ya Bakool uliopo kusini na ule wa chini wa Shabelle, ambayo ilikuwa inadhibitiwa na kundi la wanamgambo wa Al – Shabab wenye mafungamano na Al – Qaeda.
Lakini kundi hilo lilikanusha kuwepo kwa hali hiyo na kuyapiga marufuku mashirika kadhaa ya misaada ya nchi za magharibi kufanya shughuli zake katika maeneo hayo.
Baadaye ukame ulisambaa katika maeneo mengine ukiwemo mkoa wa kati wa Shabelle na Afgoye na katika kambi za watu wasiokuwa na makaazi katika maeneo yaliyokuwa yakidibitiwa na serikali katika mji mkuu Mogadishu.
Mchumi Mwandamizi wa shirika la FAO, Mark Smulders amesema, ukweli kuhusu ukubwa wa janga hilo la kibinadamu umeibuka kwenye utafiti uliofanywa kwa kushirikiana na Mtandao wa Kuonya Mapema Majanga ya Ukame, Fews Net.
“Kwa kawaida, kukadiria vifo wakati wa dharura ni sayansi isiyo rasmi, lakini kutokana na ubora na kiwango cha takwimu zilizokuwepo, tuna uhakika na utafiti huo”, amesema ofisa wa Fews Net Chris Hillbruner.
“Utafiti huo unaeleza kuwa, kilichotokea Somalia ni moja ya majanga mabaya kabisa ya ukame kuwahi kushuhudiwa katika kipindi cha miaka 25 iliyopita, “ ameongeza.
Inakadiriwa kuwa 4.6% ya jumla ya idadi ya watu na 10% ya watoto chini ya umri wa miaka mitano walifariki dunia huko maeneo ya kusini na kati mwa Somalia, imeeleza ripoti hiyo.
“Ripoti hiyo imethibitisha kuwa hatua za ziada zingechukuliwa kabla ya ukame huo haujatangazwa, amesema Phillippe Lazzarini, Mratibu wa Shughuli za Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia.
Somalia ilikumbwa na ukame mkali mwaka 2011, ulioathiri zaidi ya watu milioni 13 katika eneo lote la Pembe ya Afrika.
Maelfu ya watu walikimbia makaazi yao wakisaka chakula. Umoja wa mataifa ulitangaza ukame huo kumalizika Februari 2012.
Kwa zaidi ya miaka 20 ya vita vya weyewe kwa wenyewe, Somalia imeshuhudia wababe wa kivita wa koo, wanasiasa mahasimu na vikundi vya wanamgambo vikigombea madaraka, hali iliyoruhusu kushamiri kwa ukosefu wa utawala wa sheria.
Septemba mwaka jana, serikali inayoungwa mkono na Umoja wa Mataifa iliingia madarakani baada ya miaka nane ya utawala wa mpito, hatua iliyoleta utengamano katika baadhi ya maeneo.