Thursday, April 18, 2013

Karim Wade matatani kwa ufisadi

 18 Aprili, 2013 - Saa 12:06 GMT

Alikuwa waziri wa wizara nyingi hadi akaitwa waziri wa ardhi na anga
Mwanawe rais wa zamani wa zamani wa Senegal Abdoulaye Wade amezuiliwa na polisi baada ya kushtakiwa kwa kosa la ufisadi ambalo limehusishwa na mali anayomiliki.
Karim Wade amekanusha madai kuwa alijipatia takriban dola bilioni 1.4 kinyume na sheria wakati wa utawala wa babake.
Karim mwenye umri wa miaka 44 alikuwa waziri wakati wa utawala wa babake kutoka mwaka 2000 hadi 2012, na aliwajibika na wizara ya miundo mbinu pamoja na miradi ya kawi.
Bwana Wade anadaiwa kumiliki makampuni ya kigeni kwa njia haramu.
Alikamatwa Jumatatu, saa chache kabla ya mawakili wake kutoa stakabadhi za umiliki wa mali yake mahakamani.

'Waziri wa ardhi na anga'

Wendesha mashtaka walitangaza kuanzisha uchunguzi dhidi ya bwana Wade na mawaziri wengine watano wa zamani mwaka jana.
Hali hii ilianza kujitokeza baada ya Abdoulaye Wade kushindwa na rais Macky Sall katika uchaguzi wa Machi mwaka 2012 ambaye aliahidi kuangamiza ufisadi.
Wakati wa utawala wa miaka 12 wa Abdoulaye Wade, Karim Wade alishikilia nyadhifa kadhaa za waziri ikiwemo waziri wa miundo mbinu na usafiri wa angani.
Nyadhifa hizi zote alizoshikilia zilisababisha watu kumuita waziri wa anga na ardhi na pia ilimwezesha kusimamia kiwango kikubwa cha bajeti ya serikali

BREAKING NEWS: MILIONI 2 000,000 ZATOLEWA NA SERIKALI KUGHARAMIA MAZISHI YA BI KIDUDE

Mhe. rais wa zanzibar Dr Shein na viongozi wengine wakitoa heshima zao za mwisho mbele ya marehemu Bi Kidue kabla ya kuhifadhiwa kwenye jeneza.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa katika dua ya pamoja kumuombea Gwiji la sanaa Zanzibar Bi. Fatma Binti Baraka (Bi. Kidude) nyumbani kwake Rahaelo nyuma ya Studio ya ZBC Redio.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa pamoja na baadhi ya Familia ya Bi. Kidude wakati alipofika kutoa mkono wa pole kwa ndugu na jamaa wa msanii huyo. Kushoto kwa Balozi  ni Ndg. Haji Ramadhani Suwed na kulia ni Bw. Abdullrahman Saleh.
Umati mkubwa wa Wananchi walioshiriki mazishi ya Msanii Gwiji wa sanaa kanda ya Afrika Mashariki na Mipaka yake  Bi. Fatma Binti Baraka (Bi Kidude) nyumbani kwake Rahaleo nyuma ya Studio ya ZBC Redio.

Watoto waathirika zaidi na vita (CAR)

 18 Aprili, 2013 - Saa 11:37 GMT

Maeneo wanayopigania waasi wa Seleka
Shirika la kuwahudumia watoto la umoja wa mataifa UNICEF, limeelezea hofu ya kuongezeka kwa idadi ya watoto wanaouawa katika Jamuhuri ya Afrika ya Kati.
UNICEF linasema kuwa watoto hao wanajipata katika maeneo ya vita wakati makundi yaliyojihami yanapopambana viwanjani na hata makanisani.
Aidha shirika hilo limesema kuwa takriban watoto watatu waliuawa na wengine zaidi ya ishirini kujeruhiwa vibaya siku ya ijumaa.
Linadai kuwa watoto hao wamesajiliwa kama wapiganaji katika makundi ya waasi.
Kumekuwa na mapigano pamoja na uporaji katika mji mkuu Bangui baada ya waasi kuuteka mji mkuu mwezi jana.
Wiki tatu baada ya waasi wa Seleka kutwaa mamlaka katika mapinduzi ya kijeshi,uporaji na ghasia zimekithiri nchini humo watoto wakiwa katika hatari kubwa zaidi.
Tangu makabiliano kuanza upya mwishoni mwa mwezi wa Machi, watoto wengine wengi zaidi wamekuwa waathiriwa wa risasi wakati wengine wakisajiliwa kama wapiganaji. Pia kumekuwa na taarifa za kuongezeka kwa visa vya ubakaji
“Tunaiona nchi hii ikikumbwa na ghasia huku watoto wakiwa waathiriwa wakubwa,'' alisema Souleymane Diabate afisaa mkuu wa shirika hilo katika Jamuhuri ya Afrika ya Kati. ''Ghasia dhidi ya watoto lazima zisitishwe. Watu wasio na hatia wanauawa au kujeruhiwa na lazima zichunguzwe na maafisa wakuu,'' alisema Biabate
Wiki jana UNICEF ilitoa vifaa muhimu vya matibabu na hata kuweka kliniki ya muda kwa akina mama wajawazito ndani na nje ya mji wa Bangui. Watoto waliojeruhiwa pia wamepokea matibabu

Rais aunga mkono msamaha kwa Boko Haram

 18 Aprili, 2013 - Saa 09:20 GMT

Rais Jonathan alikuwa amepinga jambo la kuwapa msamaha wapiganaji hao
Rais wa Nigeria Goodluck Jonathan amezindua kamati mpya itakayochunguza uwezo na utekelezwaji wa msahama kwa kundi la wapiganaji wa kiisilamu Boko Haram.
Kamati hiyo itakuwa na siku sitini kufikia uamuzi wake wa mazungumzo na kuwapokonya silaha wapiganaji hao , kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa ofisi ya rais.
Pia itaangazia nyenzo za kuwasaidia waathiriwa wa ghasia ambazo chanzo chake ni wapiganaji hao.
Boko Haram limewaacha maelfu wakiwa wamefariki kutokana na ghasia ambazo wamekuwa wakisababisha mara kwa mara tangu mwaka 2009.
Kamati hiyo ambayo wanachama wake 25 wanajumuisha maafisa wa kijeshi, wasomi na wanasiasa watajaribu kuangazia sababu zinazopelelea makundi kama Boko Haram kuafanya uasi na njia za kuwazuia.
Zaidi ya hayo, rais Jonathan ameidhinisha kuundwa kwa kamati nyingine ya serikali kuhusu kuwapokonya wapiganaji hao silaha katika jitihada zake za kuimarisha usalama na uthabiti wa nchi.

Hatua mwafaka

Viongozi wa kisiasa na kidini, kutoka Kaskazini mwa Nigeria, ambalo ndio kitovu cha uasi huo, hivi karibuni walipendekeza serikali kutoa msamaha kwa wapiganaji hao.
Rais Goodluck Jonathan alijibu kauli hiyo na mwanzoni mwa mwezi Aprili alikipa kikundi cha washauri wa usalama jukumu la kuangalia ambavyo msamaha unaweza kutolewa kwa wapiganaji hao.
Duru zinasema kuwa hoja hii ya msamaha ni muhimu kwani rais alikuwa ameipuuza mwanzoni.
Ni wazi kuwa rais ameitikia kuwa juhudi za kijeshi dhidi ya wapiganaji hao hazijazaa matunda.
Hata hivyo haijulikani ambavyo wapiganaji hao watatizama wazo la rais ikizingatiwa kuwa ni makundi mengi ya mirengo tofauti ya wapiganaji.
Wiki jana Boko Haram, ambao wanataka utawala wa kiisilamu Kaskazini mwa nchi limekataa pendekezo la msamaha kwao.