Friday, June 7, 2013

Hospitali za Kenya zachelewa kutekeleza agizo la msamaha wa ada ya uzazi

Chini ya agizo la serikali mpya, huduma za uzazi kwa sasa ni bure katika hospitali za umma, vituo vya afya na kwenye kliniki nchini Kenya, lakini baadhi ya vituo vya kutoa huduma za afya bado havifuati agizo hili la msamaha wa ada zinazohusiana na uzazi.
"Serikali yangu imefanya mipangilio ya bajeti inayotosha kuwezesha akina mama wote wajawazito kupata huduma za uzazi bure katika vituo vya afya vya umma, kuanzia tarehe 1 Juni, 2013," Rais Uhuru Kenyatta alisema katika kulihutubia taifa Siku ya Madaraka, kufuatia ahadi ya kampeni ya Muungano wa Jubilee aliahidi kutekeleza wakati wa siku 100 za mwanzo madarakani.
Fedha zilizowekwa katika bajeti ya mwaka 2013-2014 zinawapa Wakenya wote fursa nzuri ya kupata huduma za msingi za afya kwenye vituo na zahanati zinazoendeshwa na serikali, rais alisema.
Kenyatta pia alifuta ada ya shilingi 10 (senti 12 ) na shilingi 20 (senti 23), ambayo zahanati na vituo vya afya vimekuwa vikitoza wagonjwa.
Hata hivyo, baadhi ya vituo vya afya vimeendelea kutoza akina mama wanaokwenda kujifungua watoto wao.
"Wakati agizo la rais linatolewa, kwa kawaida tunapaswa kusubiri waraka kutoka wizarani ukitoa maelekezo," Mrakibu wa Hospitali ya Mbagathi huko Nairobi Daktari Andrew Sule aliiambia Sabahi. "Wakina mama wanaokuja kujifungua watapaswa kulipa hadi tutakapopokea mawasiliano rasmi."
Idadi ya akina mama wanaoshindwa kurejea nyumbani baada ya kujifungua kwa kushindwa kulipa ada ya uzazi -- ambayo inagharimu shilingi 7,000 (dola 82) kwa ujifunguaji wa kawaida na shilingi 15,000 (dola 176) kwa huduma ya kujifungua kwa njia ya upasuaji -- wamekuwa wakiruhusiwa kurudi nyumbani kwa sababu hatimaye ada itafutwa, alisema.
Mkurugenzi wa hospitali kuu ya Garissa Musa Mohammed alisema kituo chake pia hakitakuwa na haraka ya kutekeleza agizo la rais. Ada ya kujifungua inaleta mapato mengi kwa hospitali yoyote, na fedha hizo huenda kwenye gharama za ukarabati, alisema.
"Kunapaswa kuwa na utaratibu na itifaki ya jinsi [vituo] vya uzazi vitakavyotunzwa kwa sasa ambapo ada ya uzazi imefutwa," aliiambia Sabahi. "Tangu Jumatatu, tulikuwa hatujapokea mawasiliano yoyote rasmi kuhusu matarajio ya siku zijazo."
Hata hivyo, baadhi ya hospitali zinasita kidogo kutekeleza sera mpya.
Siku ya Jumapili (tarehe 2 Juni), Jackson Mutua wa viunga vya jirani na Kayole vya Nairobi alimpeleka mke wake katika Hospitali ya Wilaya ya Mama Lucy Kibaki.
"[Huduma] za uzazi za bure nilipewa taarifa zake na mfanyakazi wa hospitali baada ya kuulizia ni fedha kiasi gani nilizokuwa natakiwa kulipia," aliiambia Sabahi.
Ufutaji wa ada ulikuja katika wakati muafaka, alisema, kwa sababu alipanga kukopa fedha kwa rafiki ili kulipia gharama. "nafanya kazi kama fundi mwashi na sikuwa na fedha wakati mke wangu [alipojisikia] uchungu," alisema. "Sasa naweza kuzingatia katika kutafuta chakula kwa ajili ya mke wangu na mtoto wangu aliyezaliwa."
Omar Mwanjama, ofisa ugani wa Baraza la taifa la Kudhibiti UKIMWI katika mkoa wa kaskazini mashariki mwa Kenya, alisema kufuta ada ya uzazi kunasaidia kupunguza maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, kwa kuwa wanawake wachache wangechagua kujifungulia nyumbani.
"Sasa, wakina mama wanaweza kwenda hospitalini ambako watasaidiwa na wataalamu," alisema.
Mbunge wa jimbo la Tarbaj Mohammed Ibrahim Elmi alisema ameyapokea maagizo, lakini itahitaji kujitoa rasmi ili kufuatilia kikamilifu.
"Katika matukio mbalimbali, maelekezo kama hayo yaligeuka kuwa kauli za kisiasa kuivutia halaiki," aliiambia Sabahi. "Ili yaweze kufuatwa, yanapaswa kuwa katika mawasiliano ya maandishi ili yatekelezwe."

No comments:

Post a Comment