Saturday, May 25, 2013

China kuchangia wanajeshi Mali

 25 Mei, 2013 

Nchi kadhaa za Afrika zimechangia wanajeshi wao kusaidia Mali
Serikali ya China imekubali kuchangia wanajeshi katika kikosi cha wanajeshi wa Umoja wa Mataifa wanaoshika doria nchini Mali.
Mazungumzo yanaendelea na zaidi ya wanajeshi 500 wa China wa kulinda amani pamoja na wahandisi huenda wakajiunga na mpango wa kulinda amani nchini Mali.
Serikali ya Mali ilipinduliwa katika mapinduzi ya kijeshi mwaka jana na wapiganaji wa kiisilamu wakaweza kudhibiti Kaskazini mwa Mali hadi wanajeshi wa Ufaransa walipowafurusha mwezi Januari.
Takriban wanajeshi 6,000 wa Afrika wanashika doria nchini Mali .
Msemaji wa Umoja wa Mataifa Andre-Michel aliambia shirika la habari la AP kuwa Kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa , kilipokea ahadi kutoka kwa nchi kadhaa ikiwemo China kuahidi kuchangia wanajeshi wao.
Kikosi hicho chenye wanajeshi, 12,600, ambacho kinatarajiwa kuanza kushika doria kabla ya uchaguzi kufanyika mwezi Julai, kitashirikisha wanajeshi kutoka, Afrika Magharibi
ambao tayari wako nchini Mali.
Maafisa wa kidiplomasia wa Umoja wa mataifa, wanasema kuwa China imekubali kuchangia kati ya wanajeshi 500 na 600 na kuitaja hatua hiyo ya China kama muhimu sana.
Hata hivyo ,msemaji wa wizara ya mambo ya kigeni ya China, Hong Lei hangeweza kuthibnitisha taarifa hii.
Ingawa aliwaambia waandishi wa habari, kuwa wanatarajia kuwa jamii ya kimataifa itaendelea kusaidia Mali kuweza kupata uthabiti na kushirikiana na kuwa China pia itahakikisha kufanya wajibu wake kuhusiana na hilo.
China ina zaidi ya walinda amani 1,800 wanaoshika doria katika mpango wa UN na huchangia idadi kubwa ya wanajeshi kuliko wanachama wengine wa baraza la usalama la umoja wa mataifa.
Hata hivyo wanajeshi wake kawaida huwa hawafanyi majukumu ya kijeshi kama mfano kupigana.

No comments:

Post a Comment