Monday, June 10, 2013

Mbunge mahakamani kwa uchochezi TZ

 
Wananchi wa mtwara hawataki gesi asilia kusafirishwa popote
Mbunge wa jimbo la Mtwara, eneo ambalo limekumbwa na vurugu hivi karibuni kusini mwa Tanzania amefikishwa mahakamani leo akituhumiwa kwa makosa ya uchochezi wa vurugu zilizo sababisha vifo vya watu watatu mwezi uliopita.
Hasnain Murji pamoja na watuhumiwa wengine 91 wamefikishwa kwenye mahakama ya wilaya ya Mtwara.
Kwa muda huu baadhi ya watuhumiwa wamepata dhamana huku wengine wakiendelea na taratibu za kukamilisha udhamini, wakati Mbunge huyo akisubiri kupandishwa kizimbani na kusomewa mashtaka yanayo mkabili.
Wananchi waliofika mahakamani kwa ajili ya kusikiliza kesi zinazowakabili ndugu na jamaa zao wamelalamikia utaratibu wa kuwazuwia kuingia mahakamani hapo.
Mbunge huyo wa Chama kinacho tawala nchini humo CCM, alikamatwa na kushikiliwa na jeshi la Polisi mkoani humo siku ya Jumamosi.
Idadi kubwa ya wananchi wa Mtwara wamekuwa katika mvutano mkali na Serikali ya Tanzania ambayo imekusudia kujenga bomba la kusafirisha gesi asilia inayopatikana mkoani humo hadi Dar es Salaam , Hatua inayopingwa na wananchi hao ambao wanadai gesi hiyo isisafirishwe na kupelekwa popote.

No comments:

Post a Comment