Tuesday, May 7, 2013

Kenya yawafunga maisha raia wa Iran

 6 Mei, 2013 - Saa 11:18 GMT

Raia wa Iran Ahmad Mohammed na Sayed Mousavi wamefungwa maisha

Raia wawili wa Iran wamehukumiwa kifungo cha maisha katika mahakama moja ya Kenya kuhusiana na mashtaka ya ugaidi.
Raia hao ni Ahmad Mohammed na Sayed Mousavi ambao walishtakiwa wiki iliyopita kwa kumiliki vilipuzi, ambavyo inaaminika vilikuwa vitumiwe kwa kufanya mashambulizi.
"mwili unanisisimka nikifikiria hasara ambayo ingesababishwa na shambulizi hilo la kigaidi," amesema jaji Kiarie Waweru Kiarie, kama linavyoripoti shirika la habari la AFP.
Hata hivyo, serikali ya Iran imekana kuhusika na mpango huyo wa kuishambulia nchi ya Kenya.
Siku ya Jumapili, balozi wa Iran nchini Kenya, Malik Hussein Givzad, amesema ubalozi utasaidia familia za washtakiwa hao kukata rufaa dhidi ya hukumu iliyotolewa.
"kama ubalozi, tunachoweza kufanya ni kuzisaidia familia za washtakiwa kukata rufaa, iwapo mawakili wanahisi kwamba hakuna ushahidi wa kutosha," amenukuliwa balozi Givzad na gazeti la Kenya Daily Nation.
"nchi ya Iran ina uhusiano mzuri wa kibiashara na Kenya. Huu ulikuwa ni mchakato wa kisheria, tunauheshimu." ameongeza kusema.
Mahakama ilibaini kwamba Mohammed na Mousavi ambao wanahusishwa na mtandao ambao unapanga njama ya kulipua mji wa Nairobi na sehemu ya pwani ya nchi hiyo Mombasa.
Jaji Kiarie amesema ameamua kuwafunga maisha kwa sababu ya vilio vya waathirika wa milipuko iliyopita vilisikika zaidi kuliko kujitetea kwao, imeripoti AFP.
Mawakili kutoka upande wa utetezi wanadai kwamba, Mohammed na Mousavi walihojiwa na maafisa wa usalama wa Israel pindi walipokuwa wanashikiliwa.
Hata hivyo, upande wa mashtaka umekana tuhuma hizo.

No comments:

Post a Comment