Wednesday, May 1, 2013

Afrika Kusini yakosoa Uingereza

 1 Mei, 2013


Waziri wa maendeleo ya kimataifa Justine Greening alitoa tangazo hilo kwenye mkutano mjini London
Serikali ya Afrika Kusini imekosoa Uingereza kwa tangazo lake kuwa itasitisha msaada wa moja kwa moja kwa nchi hiyo ifikapo mwaka 2015.
Mawaziri nchini Uingereza, wamesema kuwa uhusiano wao na Afrika Kusini unapaswa kuzingatia zaidi biashara wala sio maendeleo.
Lakini Afrika Kusini imesema kuwa haikushauriwa vyema kuhusu hatua hiyo na kuwa itakuwa na athari kubwa kwa taifa hilo.
Mpango wa msaada kwa nchi hiyo huwa ni pauni milioni kumi na tisa kila mwaka na unalenga zaidi kupunguza vifo vya akina mama wajawazito wanapojifungua pamoja na kuimarisha biashara.
Mnamo mwaka 2003, Afrika Kusini ilipokea pauni milioni arobaini kama msaada kwa nchi hiyo.

'Ushirikiano wa pamoja'

Waziri wa maendeleo ya kimataifa, Justine Greening, alitoa tangazo hilo katika mkutano wa mawaziri wa Afrika pamoja na wafanya biashara wakuu mjini London siku ya Jumanne.
"Afrika Kusini, imepiga hatua kubwa katika kipindi cha miongo miwili iliyopita, kiasi kuwa sasa in uchumi mkubwa katika kanda ya Afrika Kusini pamoja na mshirika mkubwa wa kiuchumi waUingereza,'' alisema Bi Greening
"tunafurahia kazi ambayo Uingereza imeifanya kwa ushirikiano na Afrika Kusini , kusaidia katika kipindi cha mpito kutoka kwa serikali ya ubaguzi wa rangi hadi sasa nchi hiyo iko kwenye mfumo wa demokrasia,'' aliongeza kusema Bi Greening
Alisema wamekubaliana kuwa Afrika Kusini sasa iko katika nafasi nzuri kuweza kufadhili miradi yake.

'Usaliti'

Lakini Afrika Kusini inasisitiza kuwa hapakuwa na mashauriano ya kina kuhusu hatua hiyo.
Taarifa kutoka katika wizara ya mashauriano ya kigeni ilisema kuwa huu ni uamuzi mkubwa sana ambao una athari kubwa,na unatosha kugeuza mkondo wa uhusiano kati ya nchi hizo mbili.
Taarifa hiyo ilisema kuwa Uingereza ingeifahamisha Afrika Kusini kuhusu hatua hiyo kupitia kwa njia rasmi za kidiplomasia.
Na kwa kujibu malalamiko hayo, Uingereza ilisema kuwa ilikuwa tayari imewasiliana na maafisa wa Afrika Kusini kwa muuda mrefu na kufanya mikutano mingi kuhusu hatua hiyo.

No comments:

Post a Comment