Sunday, April 14, 2013

Iraq yakusudia kuanzisha chuo cha mafuta na gesi Tanzania

 
 
 
 
 
 
Rate This

Balozi wa Iraq Kanda ya Afrika Mashariki   Dr. Adel Mustafa Kamil akisalimiana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi  Ofisini kwake Vuga.
Balozi wa Iraq Kanda ya Afrika Mashariki Dr. Adel Mustafa Kamil akisalimiana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Ofisini kwake Vuga.

Serikali ya Iraq inafikiria wazo la kuanzisha chuo cha mafunzo ya Taaluma ya uchimbaji wa mafuta na gesi ndani ya Jamuhuri ya Muungano  wa  Tanzania katika azma yake ya kuimarisha uhusiano wa muda mrefu kati ya pande hizo mbili.
Balozi wa Iraq katika kanda ya Afrika Mashariki   Dr. Adel Mustafa Kamil ambaye makao makuu yake yapo Mjini Nairobi Nchini Kenya alisema Iraq imeamua kufungua ukurasa mpya wa mawasiliano na marafiki zake ikilenga zaidi mataifa ya Bara la Afrika.
Akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi hapo Ofisini kwake Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar Balozi wa Iraq katika Kanda ya Afrika Mashariki  Dr. Adel Mustafa alisema hatua hiyo itaweza kuijengea Uwezo Tanzania ambayo tayari imeshaonyesha dalili za kuwa na rasilmali hiyo.
Alisema wakati Tanzania inajiandaa kuwa na muelekeo wa uchumi mpya  ni vyema mipango hiyo ikaenda sambamba na upatikanaji wa wana taaluma wazalendo watakaokuwa na uwezo kamili wa  kuendesha miradi hiyo kitaalamu.
Hata hivyo Balozi Adel Mustafa alishauri kwamba itapendeza zaidi iwapo baadhi ya wanafunzi hao wakapatiwa mafunzo ya mwanzo Nchini Iraq ili kupata taaluma  ya nadharia na ile ya vitendo.
Balozi huyo wa Iraq Kanda ya Afrika ya Mashariki  Dr. Adel Mustafa alifahamisha kwamba Iraq imepita  katika kipindi kizito cha vita kilichopelekea kulega lega kwa uhusiano wake na Mataifa mengi Duniani.
Dr. Adel Mustafa alisema hatua inayoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Iraq hivi sasa ni kuwatumia Viongozi na maafisa wake kuhakikisha uhusiano wake na nchi rafiki unarejea kama kawaida.     
Katika kuendelea kudumisha uhusiano wa pande hizo mbili Balozi Adel Mustafa ametoa ombi maalum kwa Viongozi wa Juu wa Serikali zote mbili ile ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na ya Mapinduzi ya Zanzibar kufanya ziara maalum  Nchini Iraq kwa lengo la kudumisha uhusiano huo.
“ Tunaanza kufarajika hatua kwa hatua kufuatia maombi tunayopokea kutoka kwa mataifa yanayohitaji  watendaji na wananchi wao kupatiwa fursa za masomo Nchini Iraq “. Alifafanua Dr. Adel Mustafa Kamil.
Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alimueleza Balozi wa Iraq Kanda ya Afrika Mashariki na Kati Dr. Adel Mustafa Tanzania imefarajika kuona Iraq imerejea tena katika hali ya utulivu na amani.
Balozi Seif alisema migogoro ya kisiasa inayotokea au kubuniwa na baadhi ya watu wakorofi popote pale duniani mara nyingi husababisha  kuwakosesha  haki zao wananchi walio wengi.
Alieleza kwamba amani ni muhimu na bila ya hilo hakuna maendeleo. Hivyo wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa jumla wanatarajia kwamba amani waliyonayo Wairaq itawapa fursa ya kupiga hatua zaidi katika kuimarisha uchumi wake.
“ Tanzania ilishtuka  kidogo kutokana na mitihani iliyoipata nchi ya Iraq. Lakini  hivi sasa tumefarajika kusikia na wakati mwengine kuona katika mitandao kwamba Iraq imerejea katika hali ya amani kama kawaida yake “. Alisisitiza Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimfahamisha Balozi huyo kwamba Zanzibar inahitaji  zaidi  kupata fursa za taaluma katika kuwaendeleza wananchi wake hasa katika sekta ya mafuta na Gesi.
Balozi Seif alisema Taifa la tayari limekuwa na uzoefu na kupiga hatua kubwa katika taaluma ya  masuala ya mafuta na gesi.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

No comments:

Post a Comment