Saturday, July 20, 2013

Hotuba ya kwanza ya rais Adly Misri


Chama cha Muslim Brotherhood nchini Misri kimetoa wito kwa mamilioni ya watu kushiriki maandamano mengine dhidi ya hatua ya jeshi la nchi hiyo kumpindua kiongozi aliyechaguliwa Mohamed Morsi.
Katika taarifa yake, kiongozi wa Muslim Brotherhood Mohamed Badie, ametoa wito kwa jeshi kufikiria upya hatua yake na likubali wanachotaka watu.
Lakini katika hotuba yake ya kwanza tangu kuwa kaimu rais, Adly Mansour, ameahidi kuimarisha usalama na utulivu dhidi ya wale wanaotaka kuzusha ghasia nchini Misri
Wiki mbili baada ya jeshi kumwondoa mamlakani Mohammed Morsi, bwana Mansour alisema kuwa serikali yake itajitolea kuhakikisha kuna usalama na uthabiti.
Wakati huohuo, chama cha Muslim Brotherhood kimekataa kujiunga na baraza la muda la mawaziri lililotangazwa wiki hii.
"tunapitia kipindi kigumu, na baadhi wanataka vurugu ilihali tunataka kusonga mbele,'' alisema kaimu kiongozi wakati akitoa hotuba kwenye televisheni.
"tutapigana vita vya kuhakikisha kuna usalama na tutalinda mapinduzi.''
Bwana Morsi aliondolewa mamlakani tarehe tatu mwezi Julai katika kile wafuasi wake walisema ni mapinduzi ya kijeshi.
Jeshi hata hivyo linasema kuwa lilikuwa linatimiza mahitaji ya watu baada ya mapinduzi ya kijeshi.

Nigeria kuondoa wanajeshi wake Mali


Jeshi la Nigeria
Nigeria inapanga kuondoa baadhi ya wanajeshi wake, kati ya 1,200 kutoka jeshi la kulinda amani la Umoja wa Mataifa nchini Mali, Rais wa Ivory Coast Alassane Ouattara ametangaza.
Rais Ouattara ambaye ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Uchumi ya Nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS, amesema wanajeshi hao wanahitajika nyumbani kukabiliana na wanamgambo wa Kiislam.
Haijafahamika bado ni vikosi vingapi vya Nigeria vitabakia Mali, ambako uchaguzi mkuu unatarajiwa kufanyika tarehe 28 Julai.
Wanajeshi wa Nigeria ni sehemu ya jeshi la Afrika lenye askari 12,600 ambao walichukua jukumu la kulinda amani kutoka kwa Ufaransa Julai mosi mwaka huu.
Vikosi vya Ufaransa na Afrika viliwatimua wanamgambo wa Kiislam kutoka kaskazini mwa Mali Februari mwaka huu.
Jeshi la Umoja wa Mataifa sasa linashirikiana na jeshi la Mali kulinda usalama kwa ajili ya uchaguzi. Linatarajiwa kuongezeka hadi kufikia askari 11,200, pamoja na polisi 1,400 ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.
Akizungumza kwenye mkutano wa viongozi wa mataifa ya Afrika Magharibi, katika mji mkuu wa Nigeria, Abuja, Rais Ouattara amesema kuondolewa kwa wanajeshi hao kunatokana na matatizo ya ndani nchini Nigeria.
“Hawataondoa wanajeshi wote. Sehemu muhimu ya vikosi hivyo itabakia Mali,” amesema.
Zaidi ya watu 2,000 wameuawa tangu wanamgambo wa Kiislam wa kundi la Boko Haram walipoanzisha uasi mwaka 2009 ili kuunda taifa la Kiislam katika eneo lenye Waislam wengi la Kaskazini mwa Nigeria.
Hali ya hatari ilitangazwa tarehe 14 Mei katika majimbo ya kaskazini mashariki ya Adamawa, Borno na Yobe, huku zaidi ya wanajeshi 2,000 wakipelekwa kuvunja kambi za Boko Haram na operesheni za uasi.
Uchaguzi mkuu wa mwezi huu nchini Mali una lengo la kumaliza miezi ya mtafaruku wa kisiasa ulioanza baada ya wanajeshi kumpindua Rais Amadou Toumani Toure mnamo Machi 2012, na kuruhusu waasi na wanamgambo wa Kiislam kudhibiti eneo la kaskazini mwa nchi hiyo.
Ufaransa ambayo ilikuwa mkoloni wa zamani wa mali ilipeleka zaidi ya askari 4,000 Januari mwaka huu baada ya waasi kutishia kuuteka mji mkuu wa Mali, Bamako.
Nchi za Magharibi zimeahidi kutoa msaada wa dola za Kimarekani bilioni 43 kusaidia kufufua uchumi wa Mali, ukiwa unahusishwa na utekelezaji wa mpango wa maridhiano ya kisiasa na kufanyika kwa uchaguzi mkuu.

Mateka wa MSF waachiliwa na Al shabaab


Montserrat Serra (kushoto) na Blanca Thiebaut (Kulia) walipelekwa Somalia na watekaji wao

Wahudumu wawili wa shirika la madaktari wasio na mipaka - MSF wameachiliwa huru na wapiganaji wa Al Shabaab.Wahudumu hao walitekwa nyara mwaka 2011 katika kambi ya wakimbizi wa Kisomali kaskazini mwa Kenya.
Shirika la Medecins Sans Frontieres limesema kuwa wafanyakazi hao wawili wote wako salama na wenye afya na wanatazamia sana kujiunga na jamaa zao.
Montserrat Serra na Blanca Thiebaut walitekwa nyara kutoka kambi ya wakimbizi ya Dadaab mwezi Oktoba mwaka 2011.
Kufuatia kutekwa nyara kwao pamoja na mateka wengine wa Kenya, nchi hiyo ililazimika kutuma vikosi nchini Somalia kupambana na wanamgambo wa al-shabaab.
Katika taarifa ya shirika hilo, ni afueni kubwa kwa shirika hilo kuweza kuthibitisha kuachiliwa kwa wanawake hao.
Wanawake hao walitekwa nyara tarehe 13 mwezi Oktoba mwaka 2011 na watu waliokuwa wamejihami kwa bunduki na ambao walifyatulia risasi gari la wanawake hao huku wakimjeruhi dereva aliyekuwa raia wa Kenya.
Kambi hiyo ya Dadaab ambayo ndiyo kambi kubwa zaidi duniani ya wakimbizi, inawahifadhi wakimbizi laki tano ambao wametoroka vita vya miaka mingi na njaa nchini Somalia ambayo inapakana na Somalia.
Bi Serra, ambaye ni mwalimu kutoka , Girona nchini uhispania, alikuwa mfanyakazi nchini Kenya kwa miezi miwili alipotekwa nyara. Alikuwa amefanya kazi na mashirika mengione ya misaada Amerika ya kusini na Yemen.
Moja ya magari yaliyotumiwa kuwateka nyara wafanyakazi hao

Mwanamke mwingine Thiebaut ambaye ni mhandisi wa kilimo, kutoka Madrid alikuwa ndio amekamilisha tu masomo yake ya digri katika chuo cha mafunzo ya uchumi mjini London alipotekwa nyara.
Kenya ililituhumu kundi la al-Shabab kwa kuhusika na utekaji nyara huo pamoja na matukio mengine sawa na hilo mwaka 2011 na hivyo kutishia usalama wa nchi.
Ilituma vikosi vyake nchini Somalia kuweza kupambana nao na kisha kuteka maeneo mengi ya nchi hiyo kutoka kwa kundi la al-Shabab.
Wanajeshi wake nchini Somalia sasa wamejiunga na kikosi cha jeshi katika muungano wa Afrika ambao wanasaidia serikali dhaifu ya Somalia.

Askari akamatwa kwa kudhalilisha maiti



Wanajeshi wa DRC wakitoa ulinzi katika eneo la Kanyarucinya, yapata kilomita 12 kutoka mji wa Goma.
Afisa mmoja wa jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ametiwa nguvuni baada ya kuchafua maiti za wapiganaji wa waasi nchini humo.
Waziri wa mashauri ya nchi za kigeni wa DRC, Lambert Mende, ameiambia BBC kwamba Luteni Solomo Bangala alizuiliwa jana Alhamisi na maafisa wa kijeshi baada ya mapigano kuzuka kati ya jeshi na waasi wa M23 katika eneo la mashariki karibu na mji wa Goma.
Kukamatwa kwa afisa huyo kunajiri muda mfupi tu baada ya katibu mkuu wa umoja wa mataifa Ban Ki Moon kuzungumzia madai ya kuwepo dhuluma na mateso dhidi ya wafungwa kutoka makundi ya waasi pamoja na wale waliouwawa zinazotekelezwa na wanajeshi wa Kikongomani.
Kikosi cha kulinda amani cha umoja wa mataifa kinatathmini upya hatua yake ya kuunga mkono vikosi vya serikali ya DRC kufuatia shutuma hizo.

Waasi wa M23
Mapigano kati ya jeshi la DRC na waasi wa M23 yalianza siku ya Jumapili karibu na mji wa Goma.
Mwandishi wa BBC Maud Jullien aliyepo katika mji wa Goma anasema uwanja wa mapigano ulikuwa takriban kilomita 7 katika vilima kutoka mji huo.
Hapajakuwa na mapigano yoyote katika kipindi cha siku mbili zilizopita na jeshi limesema limefanikiwa kuwafukuza waasi yapata kilomita 6, anasema mwandishi wetu.
Mwezi Novemba, wanamgambo wa M23 waliuteka kwa kipindi kifupi mji wa Goma, kisha wakaondoka baada ya kutimizia msururu wa ahadi ikiwemo kuanzisha mazungumzo na serikali.
Waasi wa M23, ambao kwa wingi wanatoka kabila la Watutsi walijiondoa katika jeshi la serikali mwezi Aprili mwaka 2012, na kuanzisha mapigano yaliyowaacha takrikaban watu 800,000 bila makao katika eneo hilo lenye utajiri mkubwa wa madini.
Mazungumzo ya amani yaliyofanyika nchini Uganda mwaka huu ili kushughulikia malalamishi ya waasi hao yamekwama.

Friday, July 19, 2013

Mapigano ya kikabila yazuka Kidal, Mali.


Wanajeshi wa Ufaransa walioko katika eneo hilo wameripotiwa kufyatua risasi hewani kutawanya makundi hayo mawili.
Wapiganaji wa kundi la waasi la MNLA nchini Mali
Machafuko hayo yanajiri wiki moja kabla ya kuandaliwa uchaguzi wa urais katika taifa hilo lililotekwa na wanamgambo wa kiislamu mwaka uliopita.
Wakati huo huo shirika la kutoa msaada, Islamic Relief, lenye makaazi yake nchini Uingereza limeonya kwamba licha ya mzozo kumalizika, eneo la kaskazini mwa Mali bado linakubwa na mkasa wa kibinadamu huku shule nyingi zikibaki kufungwa na masoko mengi kuahirishwa.
Mzozo uliopo kaskazini mwa mali umebuni kisiwa cha umaskini mkubwa katika eneo ambalo tayari limeathirika na kiangazi na uhaba wa chakula kabla ya vita kuzuka.
Shirika la Islamic Relief linasema watu milioni moja unusu sasa wanategemea chakula cha msaada , huku wengine milioni mbili wakikabiliwa na tishio la baa la njaa.
Waandamanaji wachoma magurudumu kupinga hatua ya jeshi kuingia mji wa Kidal Kaskazini mwa Mali
Hata kabla ya kampeni ya kuwatimua wanamgambo wa kiislamu iliyoongozwa na Ufaransa kuanza, takriban asilimia themanini ya chakula cha eneo hilo kilitoka maeneo ya kusini yenye rutuba nyingi au kutoka mataifa jirani ya Algeria na Libya.
Nyingi ya barabara za kufanyia biashara kuelekea kaskazini zimefungwa kutokana na hali duni ya usalama na masoko kuahirishwa. Shirika la Islamic Relief linasema vita vimesababisha uharibifu wa mfumo wa usambazaji maji huku mabomba pamoja na visima vya maji vikiharibiwa kabisa.
Shirika hilo linasema kiwango cha mateso wanayokumbana nao wakaasi wa kaskazini mwa Mali kinafumbiwa macho. Limetowa wito kwa jamii ya kimataifa kufadhili mpango wa dharura wa kutoa msaada pamoja na miradi ya maendeleo ya kudumu.
Islamic Relief limesema kuwa kwa upande wake, limetowa chakula cha msaada pamoja na mbegu kwa wakulima.

Thursday, July 18, 2013

SAKATA LA SISTA WA KANISA KATOLIKI ALIYEBAKWA NA KUNDI LA WANAUME WATATU


Sista aliye mafunzoni ametekwa na kubakwa kwa wiki nzima na kundi la wanaume watatu katika kile kinachohisiwa kuwa ni shambulio la kulipiza kisasi, vyombo vya habari nchini India vimeripoti.

Sista huyo mwenye miaka 22 alidaiwa kutekwa kwenye stesheni ya treni na binamu zake na kisha kushikiliwa mateka na kubakwa kwa zaidi ya siku kadhaa sababu waliishutumu familia yake kwa kifo cha baba yao.


Ni tukio la karibu kabisa katika mfululizo wa mashambulio ya ubakaji nchini India mwaka huu tangu mwanafunzi alipobakwa na kundi la wanaume na kufa kutokana na majeraha yake ya kutisha ndani ya basi la Delhi Desemba mwaka jana.
 

Sista huyo aliwaeleza polisi alikuwa akutane na binamu zake kwenye stesheni ya treni karibu na Chennai, huko Tamil Nadu, kusini mwa India, baada ya kudai kwamba mama yao alikuwa anaumwa.
 

Hatahivyo, anasema alichukuliwa hadi kijiji cha jirani ambako alishambuliwa mara kadhaa.
 

Watuhumiwa hao baadaye walimrejesha kwenye stesheni hiyo na kumwonya asiripoti tukio hilo.
 

Binamu wa mwanamke huyo, Jotindra Sobhasundar mwenye miaka 30, na Tukuna Sobhasundar mwenye miaka 28, walikamatwa Jumapili, kwa mujibu wa ripoti.
 

Mtuhumiwa wa tatu alikamatwa Jumatatu baada ya mfululizo wa makimbizano katika wilaya ya Kandhamal.
Vyombo vya habari za mjini humo vilisema kaka wa Sista huyo alihojiwa kuhusiana na mauaji ya mmoja wa watuhumiwa. 

 
Shambulio hilo lilidaiwa kutokea kati ya Julai 5 na 11 lakini likatangazwa hadharani wiki hii.

Tukio hilo limelaaniwa vikali na Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki nchini India.

Kardinali Oswald Gracias, alinukuliwa akisema: "Ubakaji huu wa makundi ni ugaidi wa kimwili na kihisia.

Pia alizishutumu wakala za serikali kwa 'kukwepa wajibu wao'.

HABARI ILIYOANDIKWA NA GAZETI LA "TANZANIA DAIMA" KUHUSU UDINI WA LIPUMBA YAWACHEFUA CUF

Habari iliyoandikwa na Gazeti la Tanzania Daima ikimhusisha Prof. Lipumba na udini  imewachefua  CUF  na  kuwafanya  watoe  waraka mkali wakiita Serikali kulichukulia hatua gazeti la Tanzania Daima kwa uchochezi wa kidini..
Chama    hicho  kimedai kuwa  Lengo la Gazeti la Tanzania Daima na Mwandishi wake ni kupandisha hasira za Waislam
--------------------------------------------------------------------
HUU  NI  WARAKA  WA  CUF:
CUF TUNASHANGAZWA NA JINSI SERIKALI INAVYOSHINDWA KULICHUKULIA HATUA GAZETI LA TANZANIA DAIMA KWA KUENDELEZA UCHOCHEZI WA KIDINI.

CUF-Chama cha Wananchi, kinasikitishwa sana na kitendo cha uchochezi wa Kidini unaofanywa na Gazeti la Tanzania Daima chini ya Muandishi George Maziku, kufuatia habari iliondikwa leo Tarehe 18/07/2013 toleo na 3149 . Aina hii ya uchochezi na Chuki ya Kidini anayoiendeleza bw, Maziku chini ya usimamizi wa Mmiliki wa Gazeti la Tanzania Daima na Mhariri wake, kwa maslahi ya Kisiasa tu, yatatupeleka mahala pabaya sana kama Taifa.

CUF-Chama cha Chama Wananchi tunashangazwa na tuna hoji juu ya lengo na Dhamira ya Gazeti la Tanzania Daima na Muandishi wake nini juu ya muendelezo wa habari wanayoitoa kwa muda wa miezi miwili sasa ? Habari hii ina lenga nini ? Kwamba Viongozi wa Kisiasa wanaotokana na Dini ya Kiislam hapaswi kujumuika na Waislam wenzao kwenye Nyumba za Ibada ? Au waislam hawapaswi kujadili Maendeleo ya Taifa lao ?

CUF-Chama cha Wananchi tunaona Lengo la Gazeti la Tanzania Daima na Muandishi wake ni kupandisha hasira za Waislam kwa mtazamo wa Ubaguzi wa Kidini kupitia tasnia ya Habari na hivyo kuleta machafuko yasiokuwa ya lazima.

Hata hivyo ikiwa lengo ni kuondosha Dalili za Udini kwenye mambo ya Siasa, hivi Gazeti la Tanzania Daima na Muandishi wake hawakuona Waraka wa Uchaguzi wa Mwaka 2010 uliotolewa na Kanisa Katoliki na kupewa jina la IIani ya Uchaguzi wa Kanisa Katoliki ? Waraka ambao uliwataka Wakristo kuichagua Chadema na wagombea wake, Sio hivyo tu Waraka huo ulikwenda mbali zaidi na kuwatahadharisha Wakristo wasichague CUF na CCM na kuvifananisha Vyama vya CUF na CCM ni sawa na Chui waliovaa Ngozi ya Kondoo kwa Kanisa.

Waraka huo ulipingwa vikali sana na Mzee Kingunge Ngombale Mwiru. Gazeti la Tanzania Daima na Muandishi wake walikuwa wapi ? Mbona hatukuona waandike KANISA LA CHOCHEA UDINI ? Kama hiyo haitoshi, hivi Gazeti la Tanzania Daima na Muandishi wake mbona hawakumkemea wala kuandika kuhusu Askofu Kakobe alipokua anampigia debe Mgombea wa Urais kupitia Chadema 2010 tendo ambalo lilikuwa linaonyeshwa wazi wazi kupitia Star Tv.

Kama hiyo haitoshi katika uchaguzi mdogo wa madiwani uliofanyika jijini Arusha na Chadema kushinda wafuasi na viongozi wake kutuma ujumbe mfupi wa simu (SMS) kuwa YESU AMESHINDA hilo nalo hukuliona?

Kama hiyo pia haitoshi ? Mwaka huu Mery Nagu amekwenda kusali Kanisani na kuwataka Wakristo wajitokeze kwa wingi kutoa maoni yao kuhusu katiba mpya na kuwataka waumini hao wapinge mambo yote yanayotakiwa na kikundi kidogo cha baadhi ya watu kwa maslahi ya Kanisa, je huu haukuwa UDINI ? Lowasa kila kukicha yupo Makanisani na Misikiti na anatoa Fedha anatoa je hilo sio tatizo ?

Kwa mkusanyiko wa hoja zote hizi , CUF –Chama cha Wanainchi kinashindwa kuelewa kwanini Serikali haioni hatari inayofanywa na Gazeti la Tanzania Daima na Muandishi kwa tendo hili la Uchochezi wa Kidini ? Ikiwa Serikali iliweza kuzifungia Radio Imani na Radio Maria zote zikiwa zinarusha matangazo yake kwa Malengo ya Kuendeleza Dini zao, inashindwaje kulitazama Gazeti hili la Tanzania Daima ? Hivi Serikali inasubiri nini ? mpaka hao Waislam wanaotumiwa kuwa wadini waje juu na kuleta vurugu ? Ni busara kwa Serikali kulitazama jambo hili kabla halijalet madhara.

CUF-Chama cha Wananchi kinaishauri Serikali kulitazama kwa makini jambo hili, kabla halijaleta madhara, uandishi wa aina hii ndio uliosababisha Mauaji ya Kimbali. Uandishi wa Uchochezi unaolenga kuligawa Taifa kwa misingi ya Ukabila au Udini ni uandishi hatari sana kwa Taifa letu.

Bahati mbaya Tanzania Daima hawajui au wamesahau kwamba kwa chuki ya Kidini wanayojitahitahidi kuipandikiza ndani ya Taifa letu kwa nguvu ya Tasnia ya Habari, haitawaacha SALAMA wao kama Gazeti wala Muandishi wa Habari hiyo ya Uchochezi na wanapaswa kutambua kwamba kwa kufanya hivyo tu, basi wanainunua hatari ya Taifa letu kwa gharama kubwa.

Malengo ya Kisiasa yasije kulisambaratisha Taifa letu eti kwa sababu tu Chadema ichukue Nchi. Mnaweza kufikia Lengo la kuchukua Nchi kwa Mtazamo na Mkakati huo wa Kidini, kama ambavyo mnaendlea kufanya, lakini mjue kwamba mtachukua Nchi isokuwa salama. Maana mtakuwa mmeigawa Nchi kwa Matabaka ya Udini.

Kama kweli wewe ni mwandishi mahiri na mpenda amani katika nchi, tafadhali soma kitabu cha KANISA KATOLIKI NA SIASA YA TANZANIA BARA KUANZIA MWAKA 1953 HADI 1985 kilichoandikwa na Dr. John C. Sivalon na uje na uchambuzi wa dini uliomo katika kitabu hicho.

CUF- Chama cha Wananchi kinalitaka Gazeti la Tanzania Daima , kuanzia Mmiliki wake, Mhariri wake na Muandishi wa Habari hizi, ambae mara huandika kwa mtindo wa Makala , mara huzipa uzito mkubwa kadri anavyoona inafaa kwa utashi wa Kisiasa au Udini wake, kujitazama upya juu ya hili wanalolitengeneza kama litaiweka Nchi yetu katika eneo salama.

Mwisho CUF-Chama cha Wananchi kinaitaka Serikali kuchukua hatua juu ya Uchochozi huu.

Imetolewa na
Abdul Kambaya, Naibu Mkurugenzi wa Habari, Haki za Bainaadam na Mahusiano ya Umma
0719 566 567

--------------------