Friday, July 12, 2013

Maandamano zaidi kufanyika Misri leo


Wafuasi wa rais wa zamani wa Misri Mohamed Morsi
Wafuasi na wapinzani wa rais wa Misri aliyeondolewa madarakani Mohamed Morsi wanajiandaa kwa maandamano makubwa mjini Cairo, huku waumini wa dini ya Kiislamu wakiadhimisha Ijumaa ya kwanza ya mwezi mtukufu wa Ramadan.
Wafuasi wa Bwana Morsi wanatarajia kuwa mamilioni ya raia wa nchi hiyo, wataendelea kuunga mkono wito wao wa kutaka Bwana Morsi kurejeshwa madarakani.
Wapinzani wa rais huyo wa zamani ambao waliandamana hadi rais huyo akaondolewa madarakani na jeshi watakusanyika katika medani ya Tahrir.
Watu kadhaa wameuawa kwenye ghasia zilizotokea tangu Morsi alipoondolewa.
Mwandishi wa BBC mjini Cairo, Jim Muir anasema vuguvugu la Muslim Brotherhood huenda liliwatenga raia wengi wakati wa utawala wa Morsi, lakini bado raia wengi wa nchi hiyo hawataki jeshi kuingilia masuala ya siasa.

Marekani kutuma ndege za kivita Misri

Siku ya Alhamisi serikali ya Marekani, ilitoa wito kwa utawala mpya wa Misri, kusitisha harakati zake za kuwakamata wanachama wa vuguvugu la Muslim Brotherhood na kuonya dhidi ya kulenga kundi lolote.
Wanajeshi wakishika doria mjini Cairo
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon vile vile ameonya utawala huo wa Misri kutotenga chama chochote cha kisiasa katika harakati za kutatua mzozo wa kisiasa unaokumba taifa hilo.
Hata hivyo msemaji wa Ikulu ya White House, Jay Carney amesema, utawala wa Washington hauamini kuwa ni lazima isitishe misaada yake ya Misri.
Marekani inatarajiwa kupeleka ndege nne za kivita aina ya F-16 nchini Misri, lakini haijathibitisha kuwa msaada huo utatolewa lini.
Serikali ya Marekani imesema, inachunguza ikiwa aumuzi huo wa jeshi la Misri kumuondoa madarakani rais Morsi ni mapinduzi ya Kijeshi kwa kuwa sheria za Marekani inazuia serikali kutoa misaada kwa nchi yoyote ambayo kiongozi aliyechaguliwa kwa njia ya kidemokrasia ataondolewa kupitia mapinduzi.
Wafuasi wa rais Morsi wamekuwa wakiandamana wiki nzima karibu na kambi ya kijeshi iliyoko Mashariki mwa mji mkuu wa Cairo, ambako wanaamini kuwa kiongozi wao anazuiliwa na maafisa wa kijeshi tangu alipoondolewa madarakani.

Marekani kutoa ndege za kivita Misri


Ndege ya kivita F-16
Marekani inaendelea na mpango wake wa kutoa ndege za kivita kwa jeshi la Misri licha ya msukosuko wa kisiasa unaokumba nchi hiyo. Hatua hii inajiri wakati Marekani ikiendelea kutathmini matukio ya wiki jana ambapo jeshi lilimuondoa madarakani Rais Mohammed Morsi.
Msaada wa kijeshi kwa Misri ungesitishwa endapo Marekani ingelitaja matukio ya wiki jana kama mapinduzi ya kijeshi. Kundi la Muslim Brotherhood linalomuunga mkono Morsi linasisitiza arejeshwe madarakani.
Wafuasi wake wamekua wakiandamana karibu na kambi kuu ya jeshi ambapo anaaminika kuuzuiliwa. Hapo Jumatatu,wafuasi wa Brotherhood 51 waliuawa kwa kupigwa risasi na jeshi wakati wanakabiliano.
Utawala wa mpito umesema kwamba Bw. Morsi anazuiliwa eneo salama na kwamba haki zake zinazingatiwa.Maafisa wa Marekani wamesema ndege mpya za kivita aina ya F-16 zitawasilishwa katika wiki chache zijazo.
Mpango wa kufadhili jeshi ulianza kutekelezwa mapema mwaka huu na jeshi inatarajia kupokea ndege 20 za kivita. Msemaji wa ikulu ya Rais amesema Marekani haitabadilisha mpango wa kufadhili jeshi la Misri, japo inaendelea kutathmini kuhusu matukio ya kisiasa. Msaada wa kijeshi nchini Misri ambao hutolewa na Marekani hufikia dola bilioni 1.3 kila mwaka.
Hapo Jumanne, kibali cha kumkamata kiongozi wa Muslim Brotherhood Mohamed Badie kilitolewa pamoja na wakuu wengine tisa wa kundi hilo. Viongiozi hao wamelaumiwa kwa kuchochea ghasia mjini Cairo ambapo zaidi ya watu 50 waliuawa na mamia kujeruhiwa.

Dola Bilioni 1.1 kujenga upya Nigeria

 
Viongozi wa Nigeria na China mjini Beijing
China imekubali kutoa mkopo wa dola bilioni 1.1 kwa Nigeria ili kufadhili ukarabati wa miundo msingi.Mkataba huu umeafaikiwa wakati wa ziara ya Rais Goodluck Jonathan mjini Beijing,ambapo alikutana na mwenyeji wake Xi Jinping.
Fedha hizi zitasaidia ujenzi wa barabara, viwanja vya ndege na kujenga miji minne na njia mpya ya reli.China inawekeza kwa kiwango kikubwa Barani Afrika ambapo pia imekua ikipata raslimali za mafuta na madini.
Nigeria inaongoza kwa kuzalisha mafuta Afrika lakini kwa miaka imekua na miundo msingi mibovu, huku mamilioni ya raia wake wakiishi kwa umasikini. Bw. Xi amesema nchi mbili zinashirikiana kwa minajili ya kuboresha maisha ya watu wake.
Rais Jonathan anaongoza ujumbe wa wawekezaji wa Nigeria huko China na ziara ya siku nne itasaidia kuleta mshikamano wa karibu wa kibiashara.
Kampuni za ujenzi za Ki-China zimeanza kujenga barabara nchini Nigeria, kwa kandarasi ya dola bilioni 1.7.China kwa upande wake inatarajia kupata mapipa laki mbili ya matufa ghafi kutoka Nigeria ifikapo mwaka 2015.

Brotherhood kuendelea na maandamano


Wafuasi wa Brotherhood
Kundi la Muslim Brotherhood limeapa kuendelea na maandamano ya amani kupinga kuondolewa madarakani kwa Rais Mohammed Morsi na jeshi la nchi. Wafuasi wa Mosri wamekua wakiandamana mjini Cairo karibu na kambi kuu ya jeshi anakoaminika amezuiliwa.
Taarifa ya Brotherhood inajiri wakati kumetolewa kibali kuwakamata viongozi wake wakuu. Hapo Jumatatu wiki hii wafuasi wa kundi hilo zaidi ya 50 waliuawa katika makabiliano na jeshi.
Huku haya yakiarifiwa Marekani imetangaza kwamba itatoa ndege za kivita aina ya F-16 kwa jeshi la Misri katika majuma yajayo. Utawala wa Rais Barack Obama inaendelea kutafakari matukio yaliyotokea Misri wiki jana.
Ufadhili wa jeshi ungesitishwa mara moja endapo mwingilio huo wa jeshi ungelionekana kuwa mapinduzi. Hapo Jumatano maafisa wa Misri walitoa kibali cha kukamatwa viongozi wa Muslim Brotherhood akiwemo kiongozi mkuu Mohammed Badie.
Viongozi hao wamelaumiwa kwa kuchochea ghasia ambapo wafuasi wao waliuawa pamoja na maafisa watatu wa usalama. Tayari ratiba ya uchaguzi mpya imetangazwa na Rais mpya anatarajiwa kuchaguliwa mwakani sawa na bunge.
Katiba itafanyiwa marekebisho na kupigiwa kura ya maoni kabla ya mwisho wa mwaka huu.Kundi la Brotherhood limepinga mpango mpya na kuapa halitashiriki mchakato wowote bila Mohammed Morsi kurejeshwa madarakani.

Tuesday, July 2, 2013

BAADA YA KUKAMILISHA ZIARA YAKE NCHINI......MFALME MSWATI WA SWAZILAND AAONDOKA



Mfalme Mswati wa Swaziland akisindikizwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda wakati alipoondoka kwenye uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam kurejea nyumbani baada ya kufungua maonyesho ya Biashara ya Kimataifa kwenye uwanja wa Mwalimu Nyerere Julai 1,2013.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akiagana na mfalme Mswati wa Swaziland ambaye aliondoka nchini baada ya kufungua maonyesho ya Kiataifa ya Biashara kwenye uwanja wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam Julai 1, 2013. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

GAZETI MAARUFU NCHINI MAREKANI LAANIKA UKATILI UNAOTENDEKA NCHINI


 
 Tanzania imekosolewa na gazeti maarufu la Marekani wakati Rais Obama akipokewa kwa nderemo na vifijo.
Gazeti hilo maarufu nchini Marekani la The New York Times, limechapisha habari za kuonesha matukio ya ukatili yanayofanyika Tanzania.
Habari hiyo iliyochapishwa katika toleo lake ya Juni 30, imeleza tukio la kuteswa na kuumiza kwa kiongozi wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Stephen Ulimboka.
Mwandishi wa habari hiyo amejaribu kunukuu kauli ya Dk. Ulimboka akieleza jinsi alivyotekwa na kuteswa kinyama kisha kutupwa kwenye Msitu wa Mabwepande.
Mwandishi huyo amesema kuwa Tanzania inaheshimika nje ya nchi kama kisiwa cha amani ndani ya ukanda wenye machafuko wa Afrika Mashariki.
Kwamba kutokana na sifa hizo, Tanzania imejizolea sifa na ufadhili wa fedha kutoka kwa mataifa mbalimbali yaliyoendelea, ikiwamo Marekani, ambayo mwaka jana
iliipatia zaidi ya dola milioni 480.
Alisema kuwa wakati Rais Obama akiwasili Tanzania makundi ya kutetea haki za binadamu na chama kikuu cha upinzani wanasema matukio ya vitisho na ukandamizaji wa wapinzani wa kisiasa yanashika kasi. “Kuna woga, si amani”.
Ananukuu kuwa waandishi wamekuwa wakishambuliwa na
mmoja aliuawa akiwa anatekeleza kazi yake ya uandishi wa habari.
Aliongeza kuwa Julai mwaka jana, serikali ililifungia gazeti huru la uchunguzi la kila wiki la Mwanahalisi, ambalo lilikuwa likiandika kwa undani kuhusu tukio la kutekwa na kuteswa kwa Dk. Ulimboka, ambalo lilihusisha uhalifu huo na serikali ya Rais Kikwete.
Kamati ya Kulinda Waandishi wa Habari yenye makao makuu yake New York nchini Marekani, wiki jana ilimtaka Rais Obama kuliibua suala la uhuru wa vyombo vya habari atakapokutana na Rais Kikwete jijini Dar es Salaam.
Gazeti hilo pia limetaja vurugu za kisiasa kuwa zilichukua sura mpya na ambayo haikutegemewa wakati bomu la kurushwa kwa mkono lilipolipuliwa katika mkutano wa
hadhara wa kampeni za uchaguzi wa madiwani wa
CHADEMA na kusababisha vifo vya watu wanne mkoani Arusha.

Serikali yapinga onyo la jeshi Misri


Maandamano dhidi ya Morsi yamekuwa yakifanyika Misri mara kwa mara
Taarifa kutoka ofisi ya rais wa Misri Mohammed Morsi imesema kuwa rais huyo atashikilia mpango wake wa kuleta maridhiano ya kitaifa ili kutatua mzozo wa kisiasa unaokabili taifa hilo.
Hilo ndilo tamko la kwanza kutoka kwa rais huyo tangu jeshi litoe makataa ya saa arobaini na nane kuwataka wanasiasa kutoka pande zote kutatua mgogoro huo.
Taarifa hiyo ya rais imesema kuwa hatua hiyo ya jeshi kuingilia kati itazua hali ya suitofahamu zaidi.
Jeshi limetoa makataa ya saa arobaini na nane kwa Morsi kutatua mgogoro wa kisiasa unaokumba taifa hilo la sivyo watachukua hatua.
Jeshi limekanusha madai kuwa makataa hayo ni sawa mapinduzi ya kijeshi.
Serikali imesema kuwa Morsi amewasiliana na rais Barack Obama kuhusu hali ya kisiasa inayoshuhudiwa Misri.
Wakati huohuo, shirika la habari la kitaifa Misri, limeripoti kuwa waziri wa mambo ya nje Mohamed Kamel Amr amejiuzulu.
Ikiwa ombi lake litakubaliwa, atakuwa mmoja wa mawaziri wengine watatno ambao wamejiuzulu kufuatia mgogoro huo wa kisiasa.
Mnamo jumapili, mamilioni walifanya maandamano wakimtaka rais ajiuzulu.
Maandamano mengine makubwa yalishuhudiwa Jumatu huku ripoti zikisema kuwa watu wanane waliuawa wakati waandamananaji walipovamia makao makuu ya chama tawala cha Muslim Brotherhood.
Wapinzani wa Morsi,wanamkosoa kwa kuweka maslahi ya chama mbele huku akiwapuuza wale wasiounga chama hicho.
Morsi alichaguliwa kama rais wa kwanza wa kiisilamu katika uchaguzi wa mwezi Juni mwaka 2012 tarehe 30 bbaada ya kushinda uchaguzi uliotazamiwa na wengi kuwa huru na wa haki baada ya mapinduzi ya kiraia yaliyomwondoa mamlakani Hosni Mubarak