Tuesday, July 2, 2013

GAZETI MAARUFU NCHINI MAREKANI LAANIKA UKATILI UNAOTENDEKA NCHINI


 
 Tanzania imekosolewa na gazeti maarufu la Marekani wakati Rais Obama akipokewa kwa nderemo na vifijo.
Gazeti hilo maarufu nchini Marekani la The New York Times, limechapisha habari za kuonesha matukio ya ukatili yanayofanyika Tanzania.
Habari hiyo iliyochapishwa katika toleo lake ya Juni 30, imeleza tukio la kuteswa na kuumiza kwa kiongozi wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Stephen Ulimboka.
Mwandishi wa habari hiyo amejaribu kunukuu kauli ya Dk. Ulimboka akieleza jinsi alivyotekwa na kuteswa kinyama kisha kutupwa kwenye Msitu wa Mabwepande.
Mwandishi huyo amesema kuwa Tanzania inaheshimika nje ya nchi kama kisiwa cha amani ndani ya ukanda wenye machafuko wa Afrika Mashariki.
Kwamba kutokana na sifa hizo, Tanzania imejizolea sifa na ufadhili wa fedha kutoka kwa mataifa mbalimbali yaliyoendelea, ikiwamo Marekani, ambayo mwaka jana
iliipatia zaidi ya dola milioni 480.
Alisema kuwa wakati Rais Obama akiwasili Tanzania makundi ya kutetea haki za binadamu na chama kikuu cha upinzani wanasema matukio ya vitisho na ukandamizaji wa wapinzani wa kisiasa yanashika kasi. “Kuna woga, si amani”.
Ananukuu kuwa waandishi wamekuwa wakishambuliwa na
mmoja aliuawa akiwa anatekeleza kazi yake ya uandishi wa habari.
Aliongeza kuwa Julai mwaka jana, serikali ililifungia gazeti huru la uchunguzi la kila wiki la Mwanahalisi, ambalo lilikuwa likiandika kwa undani kuhusu tukio la kutekwa na kuteswa kwa Dk. Ulimboka, ambalo lilihusisha uhalifu huo na serikali ya Rais Kikwete.
Kamati ya Kulinda Waandishi wa Habari yenye makao makuu yake New York nchini Marekani, wiki jana ilimtaka Rais Obama kuliibua suala la uhuru wa vyombo vya habari atakapokutana na Rais Kikwete jijini Dar es Salaam.
Gazeti hilo pia limetaja vurugu za kisiasa kuwa zilichukua sura mpya na ambayo haikutegemewa wakati bomu la kurushwa kwa mkono lilipolipuliwa katika mkutano wa
hadhara wa kampeni za uchaguzi wa madiwani wa
CHADEMA na kusababisha vifo vya watu wanne mkoani Arusha.

Serikali yapinga onyo la jeshi Misri


Maandamano dhidi ya Morsi yamekuwa yakifanyika Misri mara kwa mara
Taarifa kutoka ofisi ya rais wa Misri Mohammed Morsi imesema kuwa rais huyo atashikilia mpango wake wa kuleta maridhiano ya kitaifa ili kutatua mzozo wa kisiasa unaokabili taifa hilo.
Hilo ndilo tamko la kwanza kutoka kwa rais huyo tangu jeshi litoe makataa ya saa arobaini na nane kuwataka wanasiasa kutoka pande zote kutatua mgogoro huo.
Taarifa hiyo ya rais imesema kuwa hatua hiyo ya jeshi kuingilia kati itazua hali ya suitofahamu zaidi.
Jeshi limetoa makataa ya saa arobaini na nane kwa Morsi kutatua mgogoro wa kisiasa unaokumba taifa hilo la sivyo watachukua hatua.
Jeshi limekanusha madai kuwa makataa hayo ni sawa mapinduzi ya kijeshi.
Serikali imesema kuwa Morsi amewasiliana na rais Barack Obama kuhusu hali ya kisiasa inayoshuhudiwa Misri.
Wakati huohuo, shirika la habari la kitaifa Misri, limeripoti kuwa waziri wa mambo ya nje Mohamed Kamel Amr amejiuzulu.
Ikiwa ombi lake litakubaliwa, atakuwa mmoja wa mawaziri wengine watatno ambao wamejiuzulu kufuatia mgogoro huo wa kisiasa.
Mnamo jumapili, mamilioni walifanya maandamano wakimtaka rais ajiuzulu.
Maandamano mengine makubwa yalishuhudiwa Jumatu huku ripoti zikisema kuwa watu wanane waliuawa wakati waandamananaji walipovamia makao makuu ya chama tawala cha Muslim Brotherhood.
Wapinzani wa Morsi,wanamkosoa kwa kuweka maslahi ya chama mbele huku akiwapuuza wale wasiounga chama hicho.
Morsi alichaguliwa kama rais wa kwanza wa kiisilamu katika uchaguzi wa mwezi Juni mwaka 2012 tarehe 30 bbaada ya kushinda uchaguzi uliotazamiwa na wengi kuwa huru na wa haki baada ya mapinduzi ya kiraia yaliyomwondoa mamlakani Hosni Mubarak

Monday, July 1, 2013

Wanajeshi wa UN kuanza kazi Mali


Umoja wa mataifa hii leo umeanza kupeleka wanajeshi wake nchini Mali na kufikisha idadi ya wanajeshi wanaoshika doria nchini humo na ambao watakuwa chini ya UN hadi, 6,000.
Idadi ya wanajeshi inatarajiwa kufika 12,640 mwisoni mwa Disemba.
Umoja wa Mataifa utachukua jukumu la kushika doria kutoka kwa jeshi la Ufaransa ambalo lilisimamia operesheni ya kuwafurusha wapigananji wa kiisilamu kutoka Kaskazini mwa nchi mwezi Januari.
Jukumu lake la kwanza litakuwa kuhakikisha kuna usalama kabla ya uchaguzi wa urais kufanyika tarehe 28 mwezi huu.
Wapiganaji wa kiisilamu walianza kufanya harakati zao baada ya mapinduzi ya kijeshi yaliyomwondoa mamlakani rais wa taifa hilo huku wapiganaji wa kiisilamu wakitwa udhibiti wa eneo Kaskazini mwa nchi hiyo ikiwemo miji ya Gao, Kidal na Timbuktu ambako waliamuru kutumika kwa sheria kali za kiisilamu.
Ufaransa iliamua kuingilia mzozo huo, baada ya wapiganaji wa kisilamu kutishia kuvamia mji mkuu Bamako.
Tangu mwezi Januari, wanajeshi 4,000 wa Mali, wamechukua udhibiti wa sehemu kubwa ya miji mikubwa nchini humo, lakini wapiganaji kadhaa wamekuwa wakifanya mashambulizi ya kuvizia,
Jeshi la Umoja wa mataifa litajulikana kama Minusma na litahitaji kufanya kazi nzuri.
Harakati za jeshi la Ufaransa zimewafurahisha wengi kwa sababu wamekuwa wakitumia nguvu.
Lakini waasi wametoroka na wananchi wengi wa Mali wanahofia kuwa wanajeshi wa UN huenda wasitumie nguvu kama wanavyofanya wanajeshi wa Ufaransa.

George Bush na Obama wakutana uso kwa uso katika ardhi ya Tanzania leo


Rais wa Marekani, Barack Obama na mtangulizi wake, George W. Bush, leo wanakutana ana kwa ana kwenye ardhi ya Tanzania watakapoweka mashada kwenye Ubalozi wa zamani wa Marekani uliolipuliwa mwaka 1998.


Rais Obama ameweka rekodi ya kuwa mtu wa kwanza mweusi kuchaguliwa kuongoza Marekani, akipokea wadhifa huo kutoka kwa Rais Bush, ambaye aliiongoza taifa hilo kuanzia mwaka 2000-2008.


Kitendo cha vigogo hao kukutana nchini ni cha
kihistoria na kinadhihirisha jinsi Marekani ilivyoipa kipaumbele Tanzania kwa masuala ya diplomasia.

Viongozi hao wawili, wapo Tanzania wakati Rais Obama akimalizia ziara yake ya Afrika na Bush atakuwa na mkewe, Laura, watahudhuria mkutano wa wake za marais wa Afrika unaodhaminiwa na Taasisi ya Bush Foundation.

Pia, Michelle Obama, atahudhuria mkutano huo kabla ya kuondoka kurejea Marekani.

Balozi mbili za Marekani za Dar es Salaam na Nairobi, Kenya zilishambuliwa kwa wakati mmoja Agosti 7, 1998.

Obama ataweka shada kama sehemu ya kumbukumbu ya tukio hilo na Bush ataungana naye katika shughuli hiyo.
Hata hivyo, viongozi hao hawatahutubia wakati wa shughuli hiyo.


Rais Obama ametoa pongezi kwa sera za Bush Afrika hasa kwa kuongoza mapambano dhidi ya ugonjwa hatari wa Ukimwi.


Hata hivyo, utawala wa Rais Obama umejikita zaidi katika mapambano dhidi ya ugaidi.


Kuna kamandi ya Jeshi ya Africom, ambayo ina kazi kubwa ya kukabiliana na ugaidi barani humu.


Operesheni kubwa za Africom zipo nchi za Afrika Kaskazini, Somalia na Afrika ya Kati ambako wanamsaka kiongozi wa Kundi la Waasi la Lord Resistance, Joseph Kony.
Mwananchi

Makao ya chama kikuu yavamiwa Misri 1 Julai, 2013 - Saa 09:43 GMT



Maandamano dhidi ya rais Morsi watu wakimtaka aondoke mamlakani
Waandamanaji wanaopinga serikali nchini Misri, wamevamia makao makuu ya chama tawala cha Muslim Brotherhood mjini Cairo.
Inaarifiwa wamepora mali iliyokuwa kwenye ofisi hizo katika mji wa Moqattam wakitupa baadhi ya vitu nje ya madirisha kabla ya kuiteketeza ofisi yenyewe.
Rais Mohammed Morsi ni rais wa chama hicho cha kiisilamu chenye ushawishi mkubwa.
Awali, vuguvugu la upinzani lililoandaa maandamano hayo, ambayo yameshuhudia mamilioni ya watu wakijitokeza kuandamana nchini Misri, wametoa makataa kwa rais Morsi hadi Jumanne ajiuzulu.
Taarifa iliyotolewa na kundi hilo, Tamarud au (waasi) ilisema kuwa bwana Morsi huenda akakumbana na raia wasiotii sheria kama njia ya kumuonyesha kuwa wanampinga ikiwa hataondoka mamlakani na kuruhusu uchaguzi kufanyika.
Mamilioni ya watu walihudhuria maandamano, nchini kote Jumapili kumtaka Morsi kuondoka mamlakani.
Pande zote husika zilishangazwa na maandamano yanayofanywa dhidi ya Morsi.
Upinzani ni muungano wa vyama vingi, vikiwemo vianvyomuunga mkono rais aliyeng'olewa mamlakani Mubarak pamoja na watu waliojitolea maisha yao kumuondoa mamlakani.
Changamaoto kwano ni kutafuta njia ya kuendwel;eza maandamno yenyewe hadi wanachokitaka kitakapotimia.
Masemaji wa rais Morsi ameitisha mkutano kati ya pande husika.
Kwa hilo kufanikiwa, rais atahitajika kujitolea na kukubali matakwa yao, ikiwemo hata kufanyia katiba marekebisho.
Hakuonyesha dalili za kutaka mwafaka na wanaompinga, alipokuwa anatoa hotuiba yake wiki jana.
Kwa waandamanaji, wanataka aondoke mamlakani kwa kuitisha uchaguzi wa mapema. Kwa sasa vurugu inaonekana zitaendelea kwa muda.

Rais Barack Obama alipowasili Tanzania


Rais Barack Obama wakati wa ziara yake Afrika Kusini
Rais wa Marekani Barack Obama, amewasili nchini Tanzania katika mkondo wake wa mwisho wa ziara yake barani Afrika.
Ziara ya Obama inasemekana kulenga kuimarisha uhusiano wa kibiashara na Afrika huku kukiwa na wasiwasi kuwa Marekani inaachwa nyuma na China katika uhusiano wao na Afrika.
Obama amewasili Tanzania baada ya ziara yake ya Afrika Kusini ambako rais mstaafu Nelson Mandela anaugua.
Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete na familia yake pamoja na maafisa wake wa serikali na wacheza densi za kitamaduni walimkaribisha Obama na familia yake mjini Dar es Salaam.
Baadhi ya wananchi wa Tanzania kupitia mitandao ya kijamii wamekosoa ziara ya Obama katika nchi yao, wakisema kuwa ziara yake imeathiri shughuli za maisha yao ya kila siku.
Obama alitembelea Senegal kabla ya kupitia Afrika Kusini na kisha Tanzania ambako ziara yake ya Afrika inaishia kabla ya kurejea Marekani.
Obama ameambatana mamia ya wafanyabiashara na swala la uchumi linatarajiwa kupewa kipamboele kwenye ajenda.
Aidha Obama atatembelea kiwanda cha kuzalisha umeme kinachomilikiwa na Marekani kufuatia tangazo lake mwishoni mwa wiki wa mpango wa mabilioni ya dola kufadhili mradi wa uzalishaji wa kawi.
Mpango huo wa miaka mitano, unatarajiwa kuwezesha nchi nyingi Afrika kuweza kupata kawi kwa ushrikiano na nchi zingine za Afrika na sekta binafsi.
Wakati wa ziara yake, nchini Afrika Kusini, kiongozi huyo wa Marekani hakumtembelea Mandela ambaye anasalia kuwa mahututi hospitalini akiigua maradhi ya mapafu.
Duru zinasema kuwa barabara zimefungwa na usalama kudhibitiwa vilivyo, mjini Dar es Salaam.

Monday, June 24, 2013

Hali ya wasiwasi kuhusu afya ya Mandela

Mzee Nelson Mandela
Wananchi wa Afrika Kusini wanaelekea kazini asubuhi ya leo wakiwa na simanzi huku wakisubiri habari kuhusu afya ya rais mstaafu Nelson Mandela ambaye madaktari wanasema yuko mahututi.
Taarifa kutoka ikulu ya rais zilisema Jumapili jioni kuwa Mandela alikuwa amezidiwa ingawa madaktari wanafanya kila wawezalo kuhakikisha kuwa anapata afueni.
Afisaa mmoja mkuu alisema kuwa raia wa Afrika Kusini wasiwe na maytumaini kupita kiasi.
Mandela ambye alikuwa rais wa kwanza mweusi wa Afrika Kusini, akiwa na umri wa miaka 94,alipelekwa hospitalini mapema mwezi huu, ikiwa ni mara ya tatu kwake kulazwa hospitalini akiugua ugonjwa wa mapafu mwaka huu.
Rais Jacob Zuma alisema Jumapili kuwa alimzuru Mandela Hospitalini na kuzungumza na mkewe kuhusu hali ya rais mstaafu.
Madaktari wanaomtibu Mzee Nelson Mandela wamesema hali yake imekuwa sio nzuri kwa saa ishirini na nne zilizopita na sasa ni mahututi.
Habari hizo zimekuja kupitia taarifa iliyotolewa na ofisi ya rais ya Afrika Kusini.
Taarifa hiyo imesema bado Mzee Mandela ameendelea kusalia hospitalini mjini Pretoria kwa siku ya kumi na sita akitibiwa mapafu yaliyosababisha tatizo kwenye mfumo wake wa upumuaji.
Rais Jacob Zuma amemtembelea Mzee Mandela na pia kuzungumza na jopo la matabibu wanaomtibu.
Baadaye bwana Zuma alirejea kauli yake ya kulitaka taifa na dunia kumuombea Mzee Mandela apate nafuu.